FOR YOU 2
A Story by Elton Tonny
Familia, Urafiki, Mapenzi, Mahaba, Tamaa, Hila, Usaliti, Unyanyasaji, Uhalifu, Mauaji, Visasi, Vita, Mambo yasiyotazamiwa
R-rated 18+
Enjoy!
★★★★★★★★★★★★
SEHEMU YA SITA
★★★★★★★★★★★★
Kendrick akabaki ndani ya gari lake akitafakari na kutafakari sana, na baada ya dakika nyingi, akapata wazo lingine ambalo kiukweli halikuonekana kama lingefanikiwa. Uzuri wa Kendrick Jabari ulikuwa ni kwamba sikuzote alijitahidi sana kuyaweka kichwani mambo mengi aliyoyaona kuwa muhimu, na hiyo ilitia ndani namba za simu za watu muhimu kwake. Angeweza kukariri namba kadhaa za watu kama mama yake, Casmir, Alice, Jenerali Pingu, hasa kwa ajili ya nyakati za dharura ambazo huenda angepoteza simu na kuhitaji msaada, kwa kuwa hao walikuwa ni baadhi ya watu wake wa karibu sana. Hivyo sasa akawa akijitahidi kuikumbuka namba ya mtu mmoja, ambaye alikuwa ni yule mwanamke kutokea Ghana aliyempenda sana Kendrick, yaani Margaret.
Alijitahidi kuvuta kumbukumbu ya namba yake kwa kuwa aliiona mara nyingi pindi mwanamke huyo alipomtafuta, naye akafanikiwa kuiandika yote na kupiga. Ijapokuwa alijua huenda ingekuwa ngumu sana kumpata hasa kwa sababu alikuwa nje ya nchi, bado Kendrick alijipa matumaini kuwa angempata tu, kwa sababu sasa hakuwa na mtu mwingine wa kumpa msaada ambao ungemtoa ndani ya makucha ya wanyama wakali waliomwinda. Alijua kuendelea kuwa nchini kungeleta shida hasa kwa sababu binti ya Casmir alihitaji msaada, na kama angetafuta msaada kwa hospitali kubwa au sehemu yoyote angehatarisha uhai wa kijana huyo.
Baada ya kujitahidi sana kumtafuta mwanamke huyo, ilishindikana. Alihisi hasira mno na wasiwasi mwingi, na hata matumaini yakaanza kupotea sasa. Alianza hata kuwaza ingekuwa bora kama wangekufa tu, kwa sababu isingekuwa na maana yoyote Mungu kuwanusuru wawili hawa ili wauawe tena haraka. Alielewa vizuri kwamba Kanali Jacob na Luteni Weisiko wangetaka kuhakikisha hakuna hata mmoja wao aliyebaki, hivyo kwa sasa kilichokuwepo ilikuwa ni kutoroka nchi, lakini angewezaje kufanya hivyo bila msaada? Alihofia kutafuta mtu mwingine wa nchi hii kwa sababu ni lazima taarifa zingewafikia tu watu wale na hiyyo kumweka hata mtu huyo hatarini, kwa hiyo Margaret ndiye aliyekuwa tumaini la mwisho.
Kwa kuwa hakujua ikiwa Jenerali Pingu aliwaambia watu wengine kuhusu yeye kuwa hai au la kabla hajauawa, Kendrick akaamua kujaribu kwa mara ya mwisho kumtafuta Margaret, na ikiwa ni kama muujiza tu, simu ikaita. Aliingiwa na hamu kubwa sana, akisema kwa kurudia-rudia "pokea, pokea, pokea..." huku anapiga-piga usukani. Margaret akapokea simu, naye Kendrick akafumba macho akihisi faraja kubwa moyoni. Mwanamke huyo akauliza ni nani, na baada ya Kendrick kujitambulisha, akauliza ni nini kilichokuwa kikiendelea.
Kendrick alimweleza kila kitu alichopitia. Margaret kwa kadiri fulani alijua kuwa kwenye nchi ya "boyfriend" wake huyu kulikuwa na matatizo, lakini baada ya Kendrick kumsimulia jinsi mambo mengi yalivyomgusa vibaya, mwanamke huyo alimwonea huruma sana. Alimuuliza alikokuwa, naye Kendrick akasema amejificha sehemu ya chini ya ardhi akiwa na binti ya rafiki yake. Kendrick alimweka wazi kuhusu hali ya "Sandra," na kwamba kwa kuendelea kukaa huku angezidi kuhatarisha uhai wa mtoto, na wake pia. Alimwomba sana Margaret amsaidie kumtoa huku kisiri na kumhamishia kwenye nchi nyingine akiwa na utambulisho mwingine mpya (new identity), akimwomba pia samahani kwa kuwa uhusiano wao haukuwa ukieleweka sana kwa siku za karibuni.
Margaret hakukawia kusema kwamba angefanya yote aliyoweza ili kumtoa kwa kuwa bado alimpenda. Alimwomba uvumilivu wa siku kama mbili, naye angekuwa ameshafanya mipango ya kisiri ili kufanikisha kila kitu. Akaomba amwambie alipokuwa kihususa zaidi, naye Kendrick akafanya hivyo. Margaret alipomuuliza Kendrick ikiwa "Sandra" angeweza kuvumilia kwa muda huo, Kendrick alimwambia kwamba angejitahidi kumwangalia vyema kijana wake mpaka kufikia wakati huo.
Alimshukuru sana Margaret kwa utayari wake wa kumsaidia, naye akasema angeendelea kumsubiri. Alipomaliza kuongea naye, Kendrick akafumba macho na kuinamishia kichwa chake kwenye usukani. Alikuwa akitetemeka kwa msisimko wa faraja iliyomwingia, mpaka machozi yakakaribia kumtoka. Alishukuru Mungu kimya kimya na kutoka ndani ya gari lake ili arudi kwa "Sandra" hatimaye.
Alipoanza kuingia chini kule, alitambua kwamba mwanga wa chemli ulikuwa umezimika, naye akashuka upesi mpaka chini kwa kuwa giza lilikuwa nene haswa, na aliwaza hali ya "Sandra" pia. Akawasha tochi ya simu hiyo kumulikia mbele mpaka alipomkaribia, naye akakuta bado amefumba macho. Akaangalia upumuaji wake na joto la mwili, kisha akaichukua tochi aliyoleta Jenerali Pingu na kuiwasha. Aliona kwamba chemli iliishiwa mafuta baada ya kuichunguza, hivyo angehitaji kuiacha tochi ikiwaka. Wakati alipomgeukia "Sandra" kumwangalia tena, alishtuka kiasi baada ya kumkuta akiwa amefumbua macho yake huku akimtazama!
Macho ya Sandra (Xander) yalikuwa makavu, akimwangalia Kendrick kama mtu mwenye hasira, au mwenye nia ya kikatili kumwelekea mwanaume huyo. Lakini kwa Kendrick, ilikuwa ni sababu ya kufurahia, kwa kuwa sasa "binti" huyo alikuwa amerejesha fahamu. Akamsogelea karibu zaidi ili amwangalie, naye Sandra (Xander) akataka kumkwepa na kunyanyuka, lakini maumivu ya jeraha lake tumboni yakamfanya atoe kilio cha maumivu. Ikambidi Kendrick ajitahidi kumtuliza, lakini akawa anakataa na kulazimisha kunyanyuka huku anarusharusha mikono kama anapigana naye. Kendrick alielewa kwamba "Sandra" alikuwa akiogopa sana, hivyo akamshikilia kwa nguvu kiasi na kumwambia ni yeye, uncle Kendrick.
Xander, akiwa ndani ya mwili huu wa Sandra, alikuwa akipumua kwa presha sana, akiwa tu ametoka kuamka na picha ya mwisho kukumbukia ikiwa ni jinsi pacha wake alivyopigwa risasi kichwani. Alianza kupeleka macho yake huku na huko, lakini aliona tu giza zito na uso wa Kendrick bila kujua walipo, huku akiyahisi maumivu ya kisu tumboni mwake.
"Shhh... Sandra... usijali... uko sawa, uko sawa, usijali... niko nawe... usiogope... uncle Kendrick yuko nawe...."
Kendrick akaendelea kumbembeleza, na taratibu Xander akajitahidi kutulia. Alikuwa akimwangalia Kendrick kwa macho yenye huzuni sana, na machozi yakawa yakimtoka huku mdomo wake ukitetemeka. Kendrick aliingiwa na simanzi nzito sana kuona jinsi "binti" huyu alivyokuwa na huzuni. Sura yake iliongea mengi sana zaidi ya jinsi ambavyo angeyasema kwa mdomo. Kendrick akampangusa machozi taratibu, naye Xander akaelekeza uso wake juu na kufumba macho.
"Unahisije mwilini? Tumbo linauma sana? Unahisi kama hauna nguvu?" Kendrick akawa anamuuliza.
Xander akabaki kimya tu.
"Sandra... niambie unahisije... unaumia sana niku... eh Mungu yaani hata sijui... aam, una njaa? Nikupe juice? Au, biskuti?" Kendrick akaendelea kumsemesha.
"Sandra yuko wapi? Dada yangu yuko wapi?" Xander akauliza.
Kendrick akabaki kumtazama.
"Niko wapi? Mama... baba... Azra... Salome... wako wapi?" akauliza tena.
Kisha akafumbua macho na kumgeukia Kendrick tena.
"S..Sandra... unahitaji ku..rejesha nguvu mwilini. Ulipoteza damu nyingi, unahitaji kula. Usijali, tuko sehemu salama kwa..."
"Siwezi kuwa hapa. Mama... Sandra... familia yangu inanihitaji..."
Xander akasema hivyo huku akijaribu kunyanyuka kwa kasi, lakini akaishia kuumia tu tumboni zaidi na kulia kwa maumivu.
"Sandra, Sandra, tafadhali tulia nakuomba mwanangu...."
"No, nahitaji kwenda aagh... aahh...."
"Umeumia Sandra, nisikilize. Tafadhali tulia nikueleze kila kitu nakuomba...."
"Hapana... ni makosa yangu.... familia yangu inanihitaji... siwezi kuwaacha..."
"Sandra dear...."
"Kwa nini niliwapeleka? Ahhh... kwa nini nisingewaacha waniue tu... kwa nini niliwapelekaaa... naahh..." Xander akawa anaongea huku analia.
"Sandra dear, tafadhali usilie.... niko..."
"Ilipaswa kuwa mimi... kwa nini lakini... Sandraaa.... haikupaswa kuwa Sandra.... naahh... haapp... siwezi... I... Azra.... uncle Kendrick... niliwapelekea kifo familia yangu.... ni makosa yangu...."
Kendrick aliendelea kujitahidi sana kumbembeleza kijana huyu, akidhani ni kwa sababu tu ya huzuni kubwa aliyokuwa nayo ndiyo maana mambo mengine aliyasema bila kufikiri. Xander alilia kwa uchungu sana. Maumivu aliyohisi mwilini na tumboni hayakuweza kulingana na maumivu makali aliyokuwa nayo moyoni. Alilia mpaka akashindwa kuendelea kulia, muda huo wote Kendrick akiwa amekikumbatia kichwa chake huku akimbembeleza. Alipoanza kutoa sauti za maumivu zilizoashiria ni tumbo lake linauma, Kendrick akaanza kumhudumia haraka ili kumpoza.
Baada ya kumtulizia maumivu kiasi, Kendrick akajaribu kumpa chakula lakini akakataa kula.
"Sandra... unapaswa kula binti yangu. Unahitaji nguvu mwilini ili..."
"Sitaki kula. Kama ni kitu nachohitaji ni kuwa na familia yangu, kwa hiyo niache tu nijiunge nao," Xander akasema.
"Sandra usiongee hivyo. Nakuomba ule... la sivyo nitakulazimisha," Kendrick akasema hivyo kama kumshawishi.
Xander akafumba macho na kugeuzia tu shingo yake pembeni.
Kendrick akaweka chakula pembeni na kukaa hapo hapo karibu yake.
"Najua unaumia Alexandra... najua jinsi ilivyo ngumu kwako na... ninakuelewa. Una... hhhh... Mama yangu aliuliwa usiku huo huo mbele ya macho yangu... na mimi sikuweza kufanya lolote. Sikuzote alikuwa akinifundisha kwamba... familia inakuja kwanza kabla ya mambo mengine yote... kwa sababu hakuna kitu chochote kilicho muhimu kuliko watu wa familia uwapendao, na wanaokupenda pia. Mwanangu... tumepoteza watu tunaowapenda sana. Nafikiri kama ni kitu ambacho wangetamani kuona kinatupata sisi ambao tumebaki... ni usalama wetu. Ikiwa kuna sehemu ambayo wapo sasa hivi... basi kutuona tukiwa sawa ni kitu ambacho kitawapa amani zaidi. Ni mimi na wewe tu ndiyo tumebaki.... na hiyo inafanya sisi sasa tuwe familia Sandra. Tafadhali... nahitaji uwe na nguvu..." Kendrick akasema kwa hisia.
"Nguvu kwa ajili nini? Hakuna kitu kingine kilichobaki kwa ajili yangu. Ni bora ungeniacha tu nife," Xander akasema akiwa bado amegeukia upande mwingine.
"Sandra... ninakuahidi... tutafanikiwa kutoka hapa salama, na nitafanya yote ndani ya uwezo wangu kuhakikisha haupatwi na jambo lolote baya...."
"Mambo mabaya yameshanipata. Ni kipi kingine ambacho kinaweza kuwa kibaya kwangu?" Xander akasema.
Kendrick akabaki tu kimya.
"Sitotaka kuwa mzigo kwa yeyote. Naomba... tafadhali..... niue," Xander akamwambia.
Kendrick akakunja uso wake kimshangao. Alihisi kuchoka sana kiakili kwa sababu alikuwa amejitahidi sana kumsaidia mtoto wa rafiki yake lakini kiwango chake cha kupoteza matumaini kilikuwa kimepita matarajio yake.
"Sandra... usiseme hivyo. Nakuahidi tutatoka hapa tukiwa salama. Mungu ana makusudi yake kuniacha mimi na wewe tukiwa hai. Kwa hiyo nakuomba usikate tamaa. Ishi kwa ajili ya wapendwa wetu wote walioondolewa hapa duniani bila kosa lolote. Ishi... ili tuje tuwaonyeshe wote waliotutendea hivi kwamba siku zote malipo ni hapa hapa duniani. Mimi na wewe tutayafanya maisha yao yawe kama ndoto mbaya ambayo watatamani kuikimbia ila watashindwa. Nakuahidi Sandra... tutawaonyesha. Tutawaonyesha maumivu kama waliyotupatia sisi..." Kendrick akamwambia kwa uhakika.
Xander alikuwa anadondosha machozi huku amekaza meno yake akihisi huzuni iliyoambatana na hasira nyingi. Kendrick akakishika kichwa chake na kuanza kuzilaza-laza nywele zake kama kumbembeleza, naye Xander akafumba macho yake taratibu.
Waliendelea kukaa humo kwa muda mrefu zaidi.
★★
Baadaye, Kendrick alipojaribu kumpa chakula, alikula kidogo, na hilo likamfariji mwanaume huyo. Mara kwa mara Kendrick angejaribu kumsimulia kuhusu mambo mengi aliyofanya pamoja na Casmir kwenye muda wote waliokuwa marafiki, kutia ndani jinsi walivyoitengeneza sehemu hiyo chini ya ardhi. Xander hakuwa na jambo lolote la kuongea hasa kwa sababu bado alikuwa kwenye huzuni, naye Kendrick alimweka wazi kuwa ndani ya muda mfupi msaada wa kuwatoa mafichoni ungefika.
Yaani kwa muda wote waliokaa hapo, iliwabidi kuvumilia hali kama kubana haja kubwa kwa kuwa hakukuwa na vyoo, lakini kwa haja ndogo walitumia vyombo vipana vya vyakula vilivyobaki tupu (kwa ajili ya Xander akiwa kwenye mwili wa kike), na chupa za juice au maji (kwa ajili ya Kendrick). Xander akaendelea kujitahidi kula na kutumia dawa ambazo zingemsaidia kurejesha nguvu.
Ilipofika muda ambao Kendrick alitarajia watu wa Margaret kufika maeneo yale, akamwandaa "Sandra" na kumwacha chini huko ili yeye aende nje kusikilizia. Alienda mpaka kwenye gari lake, ambalo wakati huu lilikuwa limeanza kupaushwa kwa vumbi kali. Akaingia na kujiweka humo kusubiri. Kwa mambo yote yaliyokuwa yamempata, ingekuwa rahisi kwa yeyote kukata tamaa, lakini kilichokuwa kinampa nguvu ya kusonga mbele wakati huu ilikuwa ni "Sandra." Aliendelea tu kusubiri hapo, akitumaini Margaret angetimiza ahadi yake, na baada ya masaa mawili hivi, ahadi hiyo ikatimia.
Zilifika gari mbili nyeusi pande hizo, lakini hazikwenda moja kwa moja usawa aliokuwa yeye kwa sababu inaonekana bado watu waliokuwemo hawakutambua alikokuwa kihalisi. Zikasimama tu, naye Kendrick akawaona wanaume wanne wakishuka kutoka humo, wawili wawili kutoka kila gari, nao hawakuweza kuliona gari la Kendrick. Akaendelea tu kutulia ili kuona kama wangefanya jambo fulani kuthibitisha ikiwa walikuwa kweli upande wake au la.
Simu yake ndogo ikaanza kuita, naye akapokea. Alipowaangalia tena, akamwona mmoja wao ameweka simu sikioni, na sauti iliyosema "Hallo..." ilifuatana na midomo ya mwanaume huyo. Kendrick akajibu, na mwanaume huyo akaanza kumwambia kwa kiingereza kuwa walikuwa wameagizwa na Margaret waje kumchukua na kumtoa nje ya nchi, lakini hawakuweza kutambua alikokuwa, hivyo awaelekeze kiusahihi. Kendrick akamwambia wamsubiri hapo hapo, kisha akatoka upesi na kuanza kuwafata mpaka walipokuwa. Walipomwona, wakampa pole, naye akawaelekeza shimo lile lilipokuwa ili wakamsaidie kumtoa "binti yake."
Xander, akiwa bado chini kule, alikuwa tu akiyatafakari maneno ya mwisho ya Sandra kwake kabla hajapoteza maisha. Alisema asisahau kwamba anampenda sana, na akamwomba apambane kokote aliko ili asalimike. Jambo muhimu zaidi hapa lilikuwa kwamba Sandra alikuwa amemwomba asalimike KWA AJILI YAKE, katika maana ya kwamba akisalimika yeye itakuwa ni kama amewaokoa wote. Maneno yao waliyotumia kutiana moyo, "for me, for you," Sandra hakuweza kuyamaliza na kuishia kusema "for me" kabla hajapigwa risasi, hivyo Xander akaona ni kama alinusurika ili kuja kuyamalizia maneno yale "for you" kwa vitendo.
Sauti za watu wakiingia hapo chini polepole zilianza kusikika, naye Xander akaangalia na kumwona Kendrick pamoja na wanaume wengine wakimkaribia. Kwa kuwa hakuwafahamu, akajaribu kunyanyuka ili kujihami, lakini Kendrick akamwahi na kumtuliza, akimwambia hatimaye msaada wao ulikuwa umefika....
★★★★
GHANA
Wawili hao walitolewa nchini kwao kisiri na kusafirishwa mpaka nchini Ghana. Ilikuwa ni kama ukombozi wa aina fulani, na kilichokuwepo baada ya kuwa wamewasili huko ilikuwa ni kumpeleka Xander (akiwa kwenye mwili wa Sandra) hospitali haraka iwezekanavyo. Watu wa Margaret waliwatendea kwa upole wawili hawa kwa kuwa waliona kweli walihitaji huduma muhimu sana kwa sababu ya kuumizwa kimwili, hivyo wakawapeleka moja kwa moja kwenye hospitali kubwa ya kibinafsi ili watibiwe upesi.
Margaret Dery alikuwa mwanamke mwenye pesa na mali nyingi pia. Baba yake alikuwa ni Waziri wa mambo ya ndani nchini humo, na yeye Margaret alikuwa ni mshiriki maalumu wa Bunge katika jiji la Kumasi nyanda za juu. Alipata cheo hicho si kwa sababu ya baba yake, bali kwa kuwa alikistahili na hata kuteuliwa na Raisi wa nchi hiyo yeye mwenyewe kutokana na bidii yake katika kuleta maendeleo. Alikuwa ameongoza ujenzi wa miundombinu mbalimbali sehemu za jiji hilo na hata vijiji vya mbali, kama ujenzi wa shule kwenye vijiji vya Nandom.
Kwa hiyo mwanamke huyu alikuwa na jina kubwa nchini humo. Alikutana na Kendrick kwa mara ya kwanza wakati yeye na baba yake walipokuja nchini miaka mingi nyuma pamoja na viongozi wengine, enzi hizo Margaret bado ni kijana mdogo tu asiyekuwa na cheo chochote. Wakati huo bado Casmir na Kendrick hawakuwa na vyeo vyao vikubwa jeshini pia, lakini walikuwa kati ya vijana wenye ustadi mzuri sana katika masuala ya kijeshi. Walikuwa miongoni mwa wale waliochaguliwa kuwapa ulinzi maalumu waliokuja kufanya uzuru, na Kendrick alikuwa mmoja wa wale waliopaswa kumlinda Margaret. Kwa hiyo kuna hali fulani zilizojitengeneza na kufanya binti huyo akaanza kuvutiwa na mwanaume huyo aliyekuwa ngangali kwelikweli, nao wakajikuta wanaingia kwenye mahusiano ya kisiri ndani ya muda huo mfupi.
Margaret aliikubali show ya Kendrick kiasi kwamba akamwomba namba za simu ili hata akirudi kwao waendelee kuwasiliana. Kwa hiyo mara kwa mara Margaret angetoka Ghana na kwenda Tanzania ili tu kuwa pamoja na Kendrick, na hata wakati mwingine angempeleka nchini kwao pindi ambazo Kendrick angekuwa na likizo fupi. Ijapokuwa baadaye uhusiano wao ulififia, hasa kwa kuwa Margaret aliolewa na mwanaume mwingine, bado alionyesha kumpenda sana jamaa, na alimwambia hangemsahau hata ingawa aliolewa na mtu mwingine.
Walipowasiliana mara chache siku za karibuni kabla ya ishu za Demba Group kuzuka, Margaret angemwambia jinsi ambavyo ndoa yake ilikuwa ni maumivu tu, kwa sababu mume wake alikuwa akitoka nje pia, lakini waliiendeleza ili kuokoa jina zuri la hadharani (reputation). Kwa kipindi kirefu Kendrick alikuwa akifanya kama kumkwepa kwa sababu hiyo, lakini katika wanawake wote aliowahi kuwa nao baada ya mke wake kufa, Margaret ndiye aliyemwingia vizuri zaidi.
Kwa hiyo, ikiwa mume wake Margaret angejua kuhusiana na hili la kumpeleka Kendrick Ghana, maoni yake yangekuwa kwamba Margaret kamleta hawala yake. Lakini Margaret alikuwa makini sana kutofanya Kendrick ajulikane na watu ambao wangeanza kueneza porojo. Kendrick alipatiwa tiba kwenye sehemu za mwili wake zilizounguzwa vibaya kwa moto, ikiwemo upande wake mmoja wa uso. Jicho lake moja liliathiriwa vibaya na mvuke mkali wa moto, hivyo kuanzia hapo aliamua kuvaa lenzi ya kiziba jicho cheusi (kwa kukiweka ndani ya jicho).
Sandra (Xander) alipatiwa matibabu pia, na afya yake ikarudi kuwa vizuri. Madaktari waliomhudumia waliwaambia Kendrick na Margaret kwamba lilikuwa jambo lisilo la kawaida kwa mtu kupoteza damu nyingi na kukaa muda mrefu bila matibabu maalum kusalimika, kama ilivyokuwa kwa "Sandra." Walisema mwili wake ni kama ulikuwa na nguvu ya ziada ambayo haikueleweka, na ni nguvu hiyo ndiyo ilimfanya astahimili kwa muda mrefu. Kihalisi hiyo ilikuwa ni kani ya Xander ndani ya mwili wa Sandra ndiyo iliyofanya jambo hilo liwezekane kutokana na kuingiliana kwa miili yao.
★★★
Basi, mwaka mmoja kutokea hapo, Kendrick na Xander waliendelea kuishi huko huko Ghana kisiri. Kendrick aliunganishwa na Margaret kufanya kazi kwenye usimamizi wa kitengo fulani kidogo cha uzalishaji wa zao la Cocoa, ambazo zingesafirishwa na kuuzwa nje ya nchi. Kazi hii ilimsaidia kuingiza kipato cha kujikimu akiwa pamoja na Sandra (Xander). Kule jijini Kumasi, Margaret alikuwa na maduka kadhaa ya bidhaa kwenye soko fulani kuu, naye alikuwa ameyaweka hayo pia chini ya uangalizi wa Kendrick, bila yeyote kutambua kwamba wawili hao walikuwa na uhusiano.
Margaret alikuwa amewatafutia nyumba fulani maalum na kubwa kwenye sehemu iliyojitenga na makazi ya watu wengine, na ambayo ilizungukwa na misitu. Kulikuwa pia na sehemu eneo hilo yenye maporomoko ya maji iliyojificha sana ambayo Xander alipendelea kwenda kutulia akiwa mwenyewe. Mara nyingi Margaret angekuja kwenye nyumba hiyo kukutana na Kendrick, nao wangepeana mahaba mazito na kufurahia wakati mwingi pamoja, kisha angeondoka tena mpaka wakati mwingine. Kwa njia fulani sehemu hiyo ilikuwa kama kichali cha mapenzi yao.
Kendrick hakutaka Xander ajihusishe na kazi zozote, zaidi ya kumletea walimu fulani hapo ambao walimfundisha mambo mengi sana. Alijifunza lugha, alijifunza mbinu na mitindo mbalimbali ya maisha, naye akapanua zaidi ufahamu na utambuzi wake. Alianza kujifunza sarakasi na mitindo ya kupigana yeye mwenyewe kwa kuwaiga wataalamu wa mambo hayo kwenye vipindi fulani vya runinga. Mwanzoni ilikuwa kama kigezo tu cha kuondoa upweke, lakini baadae aliiona kuwa njia nzuri ambayo ingemsaidia kujua jinsi ya kujilinda siku za mbeleni. Kuishi ndani ya mwili wa dada yake kulikuwa na magumu mengi, lakini mwishowe alizoea. Alikuwa pia amekwishamwambia Kendrick kuhusu yeye kuwa ndani ya mwili wa pacha wake, kwa hiyo Kendrick aliendelea kujizoeza kumwona kama mwanaume badala ya mwanamke, ingawa jambo hilo lingepaswa kuwa siri.
Mwanzoni, Xander alidhani pesa ambazo Kendrick alikuwa anatumia kufanya mambo yote zilitoka kwenye biashara zake na Margaret, lakini baadae akaanza kuhisi kwamba kuna vitu Kendrick alifanya kwa kificho vilivyomletea mali nyingi ambazo alificha. Kuna wakati alikuwa akitafuta kifaa fulani ili atumie kutengeneza banda kwa ajili ya mifugo yake michache ya sungura, pale alipojikuta ameingia kwenye chumba kidogo sana kilichofungwa kwa minyororo minene na kufuri kubwa. Alijiuliza ni kwa nini hakuwahi kuiona sehemu hiyo, naye akatafuta njia ya kulifungua kufuri hilo na kufanikiwa. Aliingia na kukuta ni chumba kilichokuwa tupu kabisa, lakini kilitunza sanduku fulani dogo la chuma.
Kwa sababu ya udadisi, alilichukua na kulifungua, na hapo akapata kuona mabamba kadhaa ya dhahabu safi kabisa. Alijiuliza maswali mengi, kutia ndani ni jinsi gani "uncle" wake alikuwa amezipata dhahabu hizo, ila akaamua kulirudisha sanduku hilo na kukaa kimya tu kama hakuwahi kuliona. Lakini kwa sababu alihitaji kujua ni jinsi gani Kendrick alikuwa akizikusanya, akaanza kumfatilia kisiri mpaka alipokuja kugundua kwamba alikuwa anaziiba dhahabu hizo. Alimsikia akitoa maelekezo ya mpango wa kuiba dhahabu kwa mtu fulani, naye akafatilia hilo kisiri pia na kupata kuwaona watu hao walipozileta dhahabu hizo. Wangegawana, kisha yeye Kendrick angetunza zile alizopatiwa kwenye sanduku lile lile.
Kwa kuwa Xander hakuelewa sababu za Kendrick kufanya haya, akaamua tu kuuliza. Kendrick naye akawa mnyoofu na kumwelezea kila kitu bila kuficha lolote. Alieleza kwamba alikuwa akijikusanyia mali nyingi ili aje kuwa na nguvu kubwa sana, na lengo lake la kuitumia nguvu hiyo lilikuwa ni kuwalipa kisasi wale wote waliomsababishia yeye na Xander matatizo. Alimwambia hakuwa amesahau ahadi yake kwake kuhusiana na hilo, na hiyo ilikuwa ndiyo sehemu ya mpango wake wa kuja kurejea nchini kwao na kuwapatia maumivu wabaya wao.
Kendrick alidhani kwamba Xander angemchukulia vibaya kutokana na mambo aliyofanya, lakini akashangaa kiasi baada ya Xander kumwambia kwamba ikiwa alitaka kufanikisha hilo, basi angepaswa kutafuta watu wenye vipaji fulani ambao wangemsaidia kukusanya mali hizo haraka, na siyo kidogo kidogo. Ushauri wake huu ulimfanya Kendrick aone kuwa Xander alimuunga mkono, naye akasema angefanya kama alivyomwambia.
Kuanzia hapo, Kendrick akawa anaendelea na kazi zake za kawaida huku kweli akitafuta watu ambao wangefaa ili kusaidia kutimiza kisasi chake yeye na Xander. Kwa upande wa Xander, tokea alipojua tu kwamba Kendrick alikuwa akifanya mipango ya kulipiza kisasi, alianza kuunda mbinu zake yeye mwenyewe zenye ufundi sana, bila hata kumwambia Kendrick, ili naye aje kutumika kwenye kisasi hicho.
★★★★★★★★★★
ITAENDELEA
★★★★★★★★★★
Comments