FOR YOU 2
A Story by Elton Tonny
Familia, Urafiki, Mapenzi, Mahaba, Tamaa, Hila, Usaliti, Unyanyasaji, Uhalifu, Mauaji, Visasi, Vita, Mambo yasiyotazamiwa
R-rated 18+
Enjoy!
★★★★★★★★★★★★★★★★★
SEHEMU YA KUMI NA MBILI
★★★★★★★★★★★★★★★★★
"Hey, kama umemaliza, nakuomba utupishe," Luteni Michael akamwambia Lexi.
"S..sawa..." Lexi akajibu.
"Nitakutafuta baadaye Lexi, sawa?" Nora akasema.
"Haya."
Lexi akajibu na kuanza kuondoka. Wasiwasi ulikuwa umemwingia na wazo moja tu likawa akilini mwake; akitoka hapo, ni moja kwa moja kumtafuta Oscar ili amfiche.
"Subiri!"
Sauti hiyo ikamfanya Lexi asimame, lakini hakugeuka nyuma. Ilikuwa ni Mario. Mwanajeshi huyu akaanza kumfata Lexi mpaka aliposimama, huku wengine wakimwangalia. Akafika usawa wa uso wake akimtazama kwa umakini.
"Niangalie," Mario akasema.
Lexi akamgeukia.
"Tulishawahi kukutana mimi na wewe?" Mario akauliza.
Lexi akatikisa kichwa kukataa.
"Mario unafanya nini? We'... em' nenda," Mishashi akamwambia.
Lexi bila kukawia akaondoka haraka.
"Kuna mambo ya muhimu hapa, halafu we unakaa kuzitafutia tu balehe zako watoto," Mishashi akamwambia.
"Hamna bwana... huyo dada kama vile nilishawahi kumwona," Mario akasema.
"ACP, walinde uwapendao dhidi ya fataki," Hussein akamwambia Nora.
Nora na Luteni Michael walikuwa wamezama na Bobby kutafuta utambulisho wa "Erick," nao wakapata kujua kwamba mwanaume mwenye sura hii alikuwa anaitwa Oscar Amari, kijana fulani mfanyabiashara tu jijini hapo. Bila kukawia wakaanza kutafuta alipokuwa wakati huu, kwa njia zile zile kama walivyofanya kwa Kevin Dass.
Baada ya kujua, Luteni Michael akawaamuru Mishashi, Vedastus, Hussein, Alex na Omari waende pamoja naye kumkamata mwanaume huyo, halafu Bobby, Mario na ACP Nora wabaki hapo hapo pamoja na Nathan Masunga, na kumwambia Samuel, yule mchoraji, aondoke tu kwa kuwa msaada wake ulitosha. Nora akamwomba Luteni Michael aende pamoja nao, lakini Luteni akasisitiza kwamba ACP alipaswa kubaki hapo ili awe salama. Bila kukawia wanaume hao wakaondoka hapo kwenda kumkamata Oscar.
★★
Giza lilikuwa limeshaingia ikiwa ni saa moja sasa. Lexi alikuwa akiendesha gari lake kwa spidi zote, huku akiwa ameunganisha kifaa kile maalum kumtafuta Torres ili amjulishe Oscar kwa njia salama kwamba alikuwa hatarini. Lakini Torres akawa hajibu, kwa sababu ni ndani ya muda huo ndiyo alikuwa anakula utamu wa LaKeisha huko "chini."
Lexi alichoka. Alijua kama angewatafuta wengine kwa njia ya kawaida (kutia ndani Oscar) na kuwapa ujumbe huo, ingekuwa hatari. Pia, sikuzote Mess Makers walikuwa na vifaa vya ufatiliaji endapo shida ingetokea kwa mmoja ili kuwapa "signal" wengine waje kutoa msaada, kama kipindi kile Kevin alivyofanya, lakini kwa wakati huu Oscar hakujua kwamba shida ndiyo ilikuwa inamfata, kwa hiyo hangeweza kuwasha hiyo signal mpaka impate, na kwa kuwa Lexi aliijua tayari, hakutaka impate mapema.
Kwa hiyo alichofanya, akawasha ya kwake aliyokuwa ameifichia ndani ya pete aliyovaa kwenye kiganja cha mkono wa kulia, ili wenzake wafikiri yeye ndiyo yuko kwenye shida, na kokote alikokuwa wangewahi kutoa msaada. Kwa wakati huu, ni Mensah, Victor, na Oscar ndiyo waliokuwa Dar, hivyo Lexi akafika maeneo fulani yaliyokuwa na miti mingi pembezoni na kuirusha pete yake yenye kifaa kile cha ufatiliaji kwa nguvu sana kuelekea huko, huku akiwa bado mwendoni. Nia yake ilikuwa ni kwamba, ikiwa Oscar na wengine wangetambua Lexi amewasha signal yake na kuanza kwenda kutoa msaada, basi wangeenda mpaka sehemu hiyo alipokirusha, hii ikimaanisha kwamba kokote Oscar alipokuwa, angeondoka, kwa hiyo Luteni Michael na wenzake wangekuta hayupo kule walikomfatilia.
Lakini bado Lexi hakuwa na uhakika sana kama jambo hilo lingekuwa na matokeo yenye faida sana, kwa hiyo bado akaamua tu kwamba angekwenda kule alikojua Oscar aliishi jijini humo kuangalia kama yupo ili awahi kumtorosha, na kama asingemkuta, basi ingekuwa imekula kwao. Akaendesha gari lake mpaka kwenye hoteli aliyokaa (yeye Lexi) na kuchukua nguo zake zile maalumu kwa ajili ya mapambano, kisha akarejea kwenye gari na kuondoka, akipanga kuzivaa ndani ya gari lake mbele ya safari kwa sababu alijua Luteni Michael na wengine wangekuwa wameshaanza mwendo kumfata Oscar.
★★
"Mmm... aaah... aaahh... tam beibyyy...aiiyyaah.. ssss... ooaah...."
Hizo zilikuwa ni sauti za kimahaba kutoka kwa mwanadada mmoja mrembo, ambaye alikuwa akipewa penzi motomoto na kijana mmoja mtundu sana, ambaye hakuwa mwingine ila Oscar mwenyewe.
Ilikuwa ni saa ya raha tu kwake, akiwa na mpenzi wake wa huku Dar es Salaam akimpa show ya uhakika. Nasema mpenzi wa Dar kwa sababu Oscar alikuwa na mpenzi kila mkoa aliowahi kukanyaga, ili kama kungekuwa na mission hapa na pale, basi asingeondoka sehemu hiyo bila kuitia alama. Lakini mwanadada huyu aliyekuwa naye ndiyo aliyekuwa wa karibu zaidi kwake kwa sababu ya Oscar kukaa Dar muda mwingi kuliko mikoa mingine, na hapa walikuwa wametoka kuangalia mechi pamoja na kuja kuliwazana kimahaba katikati ya tano kwa sita.
Oscar pia alikuwa akikaa kwenye chumba cha hoteli ya kifahari upande mwingine wa jiji. Mpenzi wake huyu alikuwa mwanadada mwenye miaka 23, naye alikuwa binti wa matawi ya juu pia. Uhusiano wao ulianza hasa kwa kuwa Oscar alikuwa mwenye swagger nzuri, na hawakuwahi hata kukaa kuzungumzia maisha ya familia zao wala nini na kufurahia tu "company" ya mmoja na mwenzake kinamna hiyo. Binti huyu angemtafuta Oscar na kutumia muda pamoja naye, kisha angelambwa viwili vitatu na kurudi kwao. Alimkubali sana Oscar, huku jamaa yeye akichukulia uhusiano huu kuwa "poa tu" maana alikuwa aina ya kijana unayeweza kumwita "playboy."
Baada ya kumridhisha mrembo wake, Oscar akalala pembeni, naye binti akakilalia kifua chake. Story mbili tatu zikafuata, kisha wote wakanyanyuka kwenda kujimwagia huku wakitaniana. Lakini kwanza, Oscar akaona ni vyema akiangalia kifaa chake kilichounganishwa kwa Torres ikiwa jamaa alikuwa amemtafuta, lakini hakukuta kitu. Akaghairi hata kuangalia kifaa kingine kuona kama kuna yeyote kati ya wenzake aliyetoa signal ya kuomba msaada kwa vifaa vyao vya ufatiliaji baada ya mpenzi wake kumshurutisha awahi bafuni ili waoge wote. Ikiwa tu angekiangalia, angetambua kwamba signal ya Lexi iliwashwa, lakini hiyo ikampita.
★★
Ni wakati huu huu ndiyo Torres alikuwa amemaliza kumfikisha LaKeisha kwa mara ya nne kule "chini" kwenye maficho yao, na bado eti mwanamke huyo akataka waendelee. Torres akamtania kwa kusema hakutumia Viagra siku hiyo kwa hiyo hapo ndiyo walikuwa wamemalizana, naye LaKeisha akabaki akihisi furaha sana. Alikubali muziki wa Torres, hata akajiuliza ni kwa nini jamaa alikuwa anambania hivyo muda wote huo. Hapo ndiyo akajua kweli mambo mazuri hayahitaji haraka.
Torres akamwacha LaKeisha kitandani ili kwenda kuangalia kwenye mitambo yake mambo yoyote mapya, naye akaghafilika sana baada ya kukuta mapya mengi yenye kushtua. Lexi alikuwa amemtafuta kwa muda mrefu, naye akasikiliza maneno yake yote kwa makini na kuchoka hata zaidi. Akaangalia muda tokea jumbe hizo zilipoingia mpaka wakati huu, pale Oscar alipokuwa, na umbali kutokea kule Lexi aliposema Luteni Michael na wenzake walikuwepo, naye akapiga mahesabu ya haraka na kuona kweli alikuwa amemponza mwenziye.
Kwa wasiwasi mwingi akaanza kumtafuta Oscar kupitia kifaa kile salama, lakini hakujibu. Akawatafuta wengine, yaani Mensah, Victor na Kendrick pia, na kuwaambia yanayoendelea. Mensah na Victor wakasema kwamba walipata signal ya Lexi na walikuwa wakielekea kule alikokuwa, lakini Torres akawaelewesha kila kitu kwa kuwaambia Lexi alifanya hivyo kama njia mbadala, kwa sababu aliyekuwa hatarini zaidi ni Oscar. Kendrick alikuwa Geita akipanga mambo fulani kisiri kwa ajili ya timu yao, naye akakazia kwa Victor na Mensah kwenda alikokuwa Oscar ili wasaidie pia.
★★
Oscar alipokuja kumaliza kuoga na kuvalishana nguo na mpenzi wake, akapata sasa kuiona signal ya Lexi ya kifaa chake cha ufatiliaji. Akashangaa sana, kisha akachukua kile kingine kwa ajili ya kuwasiliana na Torres na kukuta ametafutwa muda si mrefu. Akasogea pembeni ili kumpigia Torres, lakini kikaanza kuita kabla ya yeye kupiga. Alipopokea, Torres alisema neno moja tu lililomwelezea kijana huyu mambo mengi mno:
"Run!"
Alipaswa kukimbia haraka sana.
Bila kuuliza chochote, Oscar akaifata simu yake ya kawaida na kuitolea laini zake mbili, kisha akaikanyaga-kanyaga simu hiyo na kuzivunja laini zote, naye akaenda kuzitupa ndani ya choo cha kukaa humo bafuni. Akatoka na kuwasha kifaa chake cha ufatiliaji, kisha akaanza kubeba vifaa hivyo, nguo zile maalum kwa ajili ya mapambano, na pesa zake zote, na kuziweka ndani ya begi dogo la mgongoni kisha kulivaa. Binti akawa anamshangaa kwa sababu aliona ni kama mpenzi wake anataka kukimbia.
Akamuuliza tatizo lilikuwa ni nini, naye Oscar akamwambia hivi, "Haunijui, haujawahi kuniona, hukuwahi kuja kwenye chumba hiki, na haujui niko wapi. Yeyote atakayekuuliza chochote kuhusu mimi, kataa kwamba unanijua. La sivyo Aste, maisha yako yanaweza yakawa hatarini."
Binti akashindwa kumwelewa kabisa. Oscar akambusu tu mdomoni na kumwambia aondoke hapo upesi, kisha yeye akatangulia kuondoka. Alikwenda mpaka kwenye lifti (elevator) na kuingia, kisha akaanza kushuka chini akitumaini kuondoka hapo kabla ya waliomtafuta kufika. Alipotoka ndani ya lifti kule chini, akaanza kutembea upesi kuelekea sehemu ya kutokea kwenye jengo hilo la hoteli, lakini kasi yake ikakatizwa baada ya kuwaona wanaume waliokuwa ndiyo wameingia tu hapo. Alimtambua haraka yule aliyetangulia mbele, naye alikuwa ni Luteni Michael.
Oscar akaanza kurudi nyuma kuelekea lifti tena, lakini Alex akamwona na kumtambua, naye akawaonyesha wenzake haraka. Wote wakaanza kumkimbiza, Hussein akiwa mbele kutokana na kuwa mwenye kasi zaidi, lakini hakufanikiwa kumfikia kabla milango ya lifti haijafunga na Oscar kuanza kurudi juu tena. Watu waliokuwa sehemu hiyo wakawa wanashangaa kwa kutoelewa yaliyoendelea, lakini kwa kuona tu wanajeshi wale wakiwa wameshika bastola mikononi wengi wakaanza kukimbilia upande mwingine.
Luteni Michael akamwambia Alex abaki hapo chini kuangalia Oscar angeishia ghorofa ya ngapi ili awajulishe kwa sababu walitaka kupanda ngazi, na ili kuzilinda sehemu hizo mbili za lifti ikiwa Oscar angerudi chini tena, kisha Luteni Michael pamoja na wengine wakaanza kupandisha ngazi upesi kuelekea juu. Hoteli hii ilikuwa na ghorofa 13, naye Alex akaendelea kuangalia namba kwa nje zikiendelea kupanda tu, 4... 5... 6... 7....
Lakini Oscar akiwa ndani ya lifti hiyo huku wasiwasi ukiwa umemjaa, akashtushwa na kishindo kutokea juu yake, na baada ya kuangalia akaona mlango mdogo wa juu ukifunguka na mtu fulani akiingiza mkono wake kumpa yeye ili apande. Alipomwangalia, hakumwona uso kwa sababu ya kificha uso chake, lakini akatambua ni mwenzake kwa kuwa alikuwa amevaa nguo zile maalumu kwa ajili ya mapambano ambazo kila mmoja wao alikuwa nazo, na kwa haraka akajua ni Mensah kwa sababu nguo yake ilikuwa na mstari mwekundu shingoni. Ya Lexi ilikuwa na mstari wa njano, Torres wa zambarau, LaKeisha wa pink, Victor wa kijani, Kevin wa samawati, na Oscar mweupe.
Upesi Oscar akampa mkono wake, naye Mensah akamvuta kumpandisha kwa juu huku lifti ikiendelea kupanda. Oscar akamuuliza imekuwaje mpaka mambo yakawa hivi, lakini Mensah akasema hawakuwa na muda wa kuongea sasa. Hivyo wakaendelea kusubiri mpaka lifti ifike mwisho, na baada ya kusimama, wakaanza kupanda kamba nene zilizoishikilia lifti na kuelekea juu kabisa ili watokee kwenye dari la juu la ghorofa. Kwa kuwa lifti ilipofika mwisho ilifungua milango, hapo nje tayari Luteni Michael na wenzake walikuwepo na bastola zao wakiwa wamezielekezea humo, lakini wakashangaa kutomwona Oscar humo.
Luteni Michael akamuuliza Alex kwa vifaa vyao ikiwa Oscar alirudi chini labda, lakini Alex akakanusha. Wakiwa wanajiuliza ilikuwaje, Luteni Michael akamwambia Hussein aanze kurudi chini kwa kasi yake ili kuona tu kama Oscar angepatikana huko, halafu yeye pamoja na Mishashi, Vedastus na Omari waelekee juu ya ghorofa kabisa kwa kuwa nafasi za kumkuta huko zilikuwa kubwa zaidi. Hussein akachomoka upesi kuelekea chini, naye Luteni Michael na wenzake wakaanza kuelekea juu kupitia ngazi fupi za mwisho.
Upande wa kule juu, Oscar na Mensah tayari walikuwa wamepanda na kuanza kuelekea sehemu ambayo Mensah aliitumia kupanda juu ya jengo hilo kwa nje wakati anakuja. Alikuwa ametumia vifaa fulani viwili vyenye nguvu kali sana ya sumaku kupanda (kama mtu anayetambaa vile, lakini ukutani) kupitia chuma la bomba nene upande wa nyuma wa jengo hilo, hivyo wakati wa kushuka wangeshikana mikono miwili na kutumia mikono mingine kushika vifaa hivyo ili kushuka chini kwa pamoja.
Kwa kudhani kwamba walikuwa wamemchengua Luteni Michael na wenzake, wakafika hapo na kuanza kujiandaa kushuka pale sauti ya risasi iliposikika kutokea nyuma yao.
"Tulieni hivyo hivyo!"
Sauti ya Luteni Michael ikasikika vyema kutokea nyuma yao kwa umbali mfupi. Oscar akafumba macho na kutukana kichini-chini kwa kuwa alijua hapa walikuwa wamekwisha. Kwa kujiamini, Mensah akageuka nyuma, akiwa bado haonekani sura yake, naye Oscar vilevile akageuka. Sasa wakawaona wanajeshi wale wakiwa wanawakaribia huku bastola wakizielekezea kwao.
"Mikono juu," Luteni Michael akawaamuru.
Oscar akanyanyua mikono yake, lakini Mensah hakunyanyua.
"We' ndiyo una kiburi eti?" Luteni Michael akamuuliza.
Kufikia wakati huu, Vedastus, Mishashi na Omari walikuwa wamewakaribia zaidi, nao walipowafikia wakawapiga miguuni na kuwafanya wapige magoti. Vedastus na Omari ndiyo wakaanza kushughulika kuwafunga kwa pingu mikononi kwa kuirudisha mikono nyuma, huku Mishashi akiwa bado amewaelekezea bastola.
"Hii siku ya bahati sana kwetu. Wawili kabisa!" akasema Omari.
"Hebu mtolee hiyo mask," Luteni Michael akamwambia Vedastus.
Vedastus alikuwa tu ndiyo ameushika upande wa pembeni wa kificha uso cha Mensah, pale aliposhtushwa na sauti ya maumivu kutoka kwa Luteni Michael!
Wote wakamwangalia na kumwona amedondoka chini, akiwa amepoteza fahamu, lakini mtu aliyempiga hawakumwona. Ghafla tu akatua mtu fulani hapo na kurusha visu viwili vikali kwa kasi sana vilivyowapata Vedastus na Omari sehemu za mabegani kwa pamoja. Mishashi akaelekeza bastola kwake, lakini mtu huyo akamwahi na kumpiga mikononi kwa njia fulani iliyofanya mikono ya Mishashi ilegee, kisha mtu huyo akampiga ngumi za kasi sehemu ya pembeni ya nyonga, katikati ya kifua na pembeni ya shingo, naye Mishashi akaanguka na kutulia tuli!
Jambo hili liliwashtua sana Mensah na Oscar, kwa sababu hawakuweza kumtambua mtu huyo. Alivaa nguo nyeusi mwili mzima, na uso wake ulifunikwa kwa kitu kama kofia iliyotokea nyuma ya mgongo wake (kama yale masweta yenye kofia/hood). Mdomo wake ulizibwa kwa barakoa ngumu nyeusi yenye mchoro mweupe wa meno ya simba, na kuzunguka kiunoni kwake kulikuwa na mkanda wenye visu vidogo vidogo.
Mensah na Oscar wakasimama, huku bado mikono yao ikiwa imefungwa kwa nyuma. Hawakuweza kumtambua hata kidogo. Alikuwa mgeni kabisa kwao. Vedastus na Omari wakajitahidi kunyanyuka na kuvitoa visu vile mabegani mwao, na ile tu walipokuwa wanataka kumpiga mtu huyo kwa risasi, akaruka sarakasi nyingi kuwaelekea na kuzipiga bastola zao kwa miguu. Kisha akaanza kuwapiga wawili hao kwa kasi sana na kwa kuwachanganya mno. Wote wakaanguka chini na kutulia tuli!
Mtu huyo akamgeukia Oscar, ambaye alikuwa upande wa kulia akimwangalia kimaswali, naye akamwangalia na Mensah, ambaye alikuwa kushoto kwake. Oscar na Mensah wakaangaliana, kisha baada ya kupeana ishara, wakamfata hivyo hivyo wakiwa wamefungwa ili wamshambulie. Walijitahidi kupigana naye kwa kupokezana mitindo ili kuweza kuiwekea miili yao mihimili mizuri, lakini mtu huyo akawashinda ujanja.
Oscar kwa sababu ya wepesi wake alifanikiwa kuirudisha mikono yake iliyofungwa kwa mbele kwa kuikunja miguu yake, kisha akambana mtu huyo kwa pingu sehemu ya shingo akitaka kumnyonga. Lakini mtu huyu akaigeuza nguvu ya Oscar dhidi yake mwenyewe na kumpiga ngumi zake zile za kasi, naye Oscar akadondoka chini. Mensah ndiyo bado alikuwa mzito kutokana na mikono yake kuwa kwa nyuma bado, lakini akaendelea kujitahidi kurusha chochote alichoweza.
Mtu huyo akafanikiwa kumpiga Mensah kwa njia iliyomfanya aishiwe nguvu, kisha akaanza kumfata ili ammalize. Oscar akamwahi na kuchomoa kisu chake kimoja ili amchome, lakini mtu huyo akamkwepa na kumpiga ngumi mbili za kasi katikati ya shingo yake, naye Oscar akajishika shingoni akihisi maumivu makali. Bila Oscar kutazamia, mtu huyo akakishika kichwa chake alipokuwa ameinama huku ameishika shingo bado, na kujiviringisha kwa sarakasi nyuma ya mgongo wake huku bado akiwa amekishika kwa nguvu, na hapo akawa amemnyonga Oscar!
Mwili wake ukadondoka chini kama mzigo mzito, huku kichwa chake kikiwa kimegeukia mpaka nyuma ya mgongo wake kabisa!
Mensah bado alihisi kama nguvu imemtoka, lakini aliona vizuri sana jambo lililompata mwenzake. Alihuzunika sana. Mtu huyu asiyejulikana akaanza kumfata na Mensah ili ammalize pia, na ile anataka tu kumshika, mkono wake ukavutwa nyuma kwa nguvu sana na kushtukia anapigwa teke lililompata sehemu ya taya na kusababisha aangukie pembeni. Mensah alipomwangalia aliyempiga adui huyo, akatambua ilikuwa ni Lexi, akiwa ndani ya nguo zake za mapambano.
Mtu yule akajinyanyua kwa sarakasi na kukaa mkao wa kupambana, huku Lexi akiwa anamwangalia kwa hasira sana ndani ya mask yake. Wawili hawa wakaanza kufatana, na mkono ukaanza. Mtu huyo alifikiri angeweza kumlainisha Lexi kama alivyofanya kwa wengine, lakini alikuwa amekosea sana. Lexi aliyazuia mapigo yake yote na kumfumua yeye kisawasawa. Alijua vyema jinsi ya kupigana, hivyo alijilinda dhidi ya adui huyu na kujaribu kumlipizia kisasi Oscar. Ingawa hivyo, bado adui huyu alionekana kuwa mzoefu sana na kufanikiwa kukwepa pia mapigo ya Lexi yaliyoelekea kumuua. Wote walitumia njia zote walizoweza, lakini ikawa ngoma droo.
Ni wakati huu Luteni Michael ndiyo akaanza kurejewa na fahamu, naye akawa anawaona kwa mbali wawili hao walipokuwa wanapigana. Akaiokota bastola yake na kujitahidi kuunyanyua mkono wake uliokuwa hauna nguvu sana na kuielekeza kwa Lexi, akiwa bado amelala hapo chini, kisha akafyatua risasi iliyompiga mgongoni. Ijapokuwa Lexi aliweweseka kidogo baada ya risasi hiyo kumpata, ikawa imedunda kutokana na nguo ya Lexi kuwa 'bulletproof.' Hii ikafanya adui yule asiyejulikana aanze kuruka masarakasi yake mpaka kwa Luteni Michael na kuipiga bastola pembeni, kisha akakimbilia upande uliokuwa na nyaya nene aliyotumia kufikia huko juu na kuirukia, naye akatokomea kutoka hapo.
Lexi akamtazama Oscar pale chini. Aliingiwa na simanzi nzito sana kumwona rafiki yake akiwa mbali na uhai. Luteni Michael akawa anajaribu kujinyanyua, lakini viwiko vya mikono yake vilikuwa legevu sana kiasi kwamba akawa anashindwa. Akawaona vijana wake watatu pale chini wakiwa wamelala tuli tu. Akajiuliza ni kwa nini Hussein na Alex hawakuwa wamefika huku juu tokea muda ule alipopiga risasi hewani kuwazuia Oscar na mwenzake wasitoroke, kwa kuwa walitakiwa kuwa msaada mkubwa kwao.
Lexi akamfata Oscar pale chini, akapiga magoti huku akiangalia kichwa cha kijana huyu kikiwa nyuma ya shingo yake, naye akadondosha chozi la huzuni ndani ya mask yake. Sauti za ving'ora vya magari ya polisi zikaanza kusikika zikija kutokea kule chini.
"Hey.... we have to go..."
Mensah akasikika akimwambia hivyo, naye Lexi akafumba macho na kunyanyuka. Alipokuwa anaanza kumfata Mensah, akasimama, kisha akamwangalia Luteni Michael pale chini. Luteni yeye alijua anaangaliwa lakini sura ya aliyemwangalia hakuiona, hivyo akabaki kumtazama tu pia kama anasubiri afanye jambo fulani.
Lexi alikuwa na hasira siyo mchezo, lakini hakukuwa na muda wa kuzimalizia hapa. Akalifata begi la Oscar na kulichukua, kisha akamfata Mensah na kuzifungua pingu mikononi mwake, akamsaidia kunyanyuka, nao wakaondoka hapo kupitia njia ile ile ya Mensah. Ilibidi tu Mensah ajikaze kushuka hivyo hivyo ingawa alihisi mwili wake hauna nguvu, nao wakafanikiwa kuondoka huko.
Luteni Michael akaachwa hapo anazikusanya nguvu zake ili anyanyuke. Alikuwa akijiuliza mtu huyo alimpiga jinsi gani mpaka kufanya nguvu zake zimtoke. Akiwa anajibebabeba, wakafika maaskari hapo na mabunduki yao, wakamfata na kumsaidia kunyanyuka, naye Luteni Michael akawaambia wawaangalie wenzake kama walikuwa bado wamepoteza fahamu.
Lakini ukweli ukawa ni kwamba, Mishashi, Vedastus, na Omari, hawakuwa hai tena. Luteni Michael alihuzunika sana. Akafumba macho yake na kukaa chini tena. Maaskari wenyewe wakaendelea kufanya yao juu hapo kama kuiondoa miili ya maiti, ikiwa ni saa 3 ya saa 4 usiku sasa, na kwa sababu ya msiba huu uliokuwa umewapata wenzake, Luteni Michael aliacha hata kukaza fikira kuwaambia maaskari kwamba maadui walitorokea kupitia wapi, na wawazungukie wapi.
★★
Baada ya muda fulani, waandishi wa habari kutoka vyombo kadhaa wakawa wamefika, nao wakaanza kuhojiana na maaskari. ACP Nora na Mario wakawa wamefika pia sehemu hiyo. Walijiunga na Alex na Hussein ambao nao walikuwa wamepoteza fahamu tokea muda fulani nyuma. Kujua kwamba Vedastus, Omari, na Mishashi hawakuwa hai kuliwatia simanzi pia. Wakawa wanamuuliza Luteni Michael ni nini kilitokea.
"Mlikuwa wapi?" Luteni Michael akawauliza Alex na Hussein.
"Luteni... sisi... mimi nilipofika chini sikuona lolote lile la ajabu kutokea juu, nilimkuta tu Alex pale. Ndiyo kidogo tu tukasikia mlio wa risasi..." Hussein akasema.
"Watu wakaanza kukimbia ovyo ovyo. Tukaanza kupandisha juu. Lakini tulipofika ghorofa fulani akatokea mmoja wao, akapambana nasi... akafanya tukapoteza fahamu..." Alex akamwambia.
"Huyo mmoja wao mlimwona sura?" akauliza Mario.
"Hapana... kuna... mask fulani wanavaa," akasema Hussein.
"Kwa hiyo, ni kwamba Mess Makers wamemuua huyu Oscar kwa sababu tulimtambua au?" akauliza Mario.
"Na ni kwa nini wamuue Veda, Misha, na Omari halafu wewe wakuache?" akauliza Nora.
"Kulikuwa na mtu mwingine hapa... na yeye siyo mmoja wao," akasema Luteni Michael.
Wote wakamwangalia kwa umakini.
"Alikuwa anapigana nao... lakini na yeye sikumwona... yaani... hii inachosha sana," akasema Luteni Michael.
Kifaa cha mawasiliano cha Mario kikaita, naye akasogea pembeni, akapokea na kuongea na Bobby.
"Luteni... Bobby anasema Kanali Oswald anakutafuta," Mario akamjulisha baada ya kurejea.
"Yuko wapi?" Luteni Michael akauliza.
"Amefika jengoni," Mario akasema.
"Tunapaswa tukupeleke kwanza hospitali," Nora akamwambia Michael.
"No. Tunaenda huko huko. Kanali nilikuwa nimeshamwambia kuhusu hii ishu na kumwahidi ningemletea matokeo mazuri leo leo kama exchange ndogo ya msaada wake kwa ile hacking aliyofanya Bobby..." Luteni Michael akamwambia.
"Kwa hiyo... sasa matokeo siyo mazuri... atafanya nini?" akauliza Hussein.
"Ndiyo twende ukajue," Luteni Michael akamwambia na kuanza kuondoka.
Nora, Hussein, Mario na Alex wakabaki kuangaliana, kisha nao wakaondoka hapo pia wakimfata Luteni Michael.
Mwili wa Oscar ulipelekwa kuhifadhiwa, vilevile na miili ya wanajeshi wale watatu. Timu ya Luteni Michael haikuwa na wanajeshi wa ovyo ovyo tu, walikuwa ni watu aliofanya nao kazi kwa ukaribu na kwa muda mrefu, hivyo aliwathamini sana. Vifo vya hawa watatu vilimpa pengo kubwa sana ambalo ingechukua muda mrefu kuja kuliziba. Alijilaumu pia, kama ilivyo kawaida ya mtu akifiwa, kwa kuhisi ni kama hakufanya mengi kuweza kuokoa maisha ya wenzake.
★★
Walipofika kule kwa Bobby, walimkuta Kanali Oswald Deule akiwa hapo, naye akamuuliza Luteni Michael zawadi yake ilikuwa wapi. Luteni akamweleza kila kitu, na kuomba samahani kwa kuwa mpango wake ulikuwa ni kumkamata Oscar akiwa hai, lakini sasa angempatia Oscar aliyekufa. Akamwambia kama alitaka kuwapa adhabu yoyote ile angeikubali tu, hata kama akiondolewa kwenye mission hii, kwa kuwa alihisi ni kama amepoteza muda mwingi tokea walipoanza msako huu bila kuleta matokeo yoyote mazuri.
Lakini kwa kushangaza, Kanali Oswald akamwambia asifikiri hivyo, na kwamba kiukweli kazi waliyokuwa wameifanya ilikuwa nzuri, na walitakiwa kuendelea. Wote hapo walidhani labda Kanali Oswald angewaambia waweke kituo kikuu katika msako huu, lakini ikawa tofauti. Kanali akamwambia Luteni Michael alielewa kwamba amepoteza watu muhimu kwake, kwa hiyo angetarajia aendelee na mgawo huu ili awalipizie na kisasi. Hakuna mtu mwingine aliyeweza kufika hadi kwenye hatua ya kumkamata Kevin Dass na Oscar Amari isipokuwa Luteni Michael na timu yake, hivyo Kanali Oswald akawaambia wangeendelea na kazi zaidi baada ya kufanya msiba kwa ajili ya wanajeshi wake. Akamwahidi pia kwamba msiba huu ungefanywa kitaifa ili kuwaenzi wanajeshi hao, na ili kuwaonyesha watu jinsi Mess Makers walivyo watu wabaya sana.
Baada ya hayo, Kanali Oswald akamwita Luteni Michael pembeni ili waongee. Alimkumbusha kwamba kwenye msako huu, alipaswa kuwa mwangalifu sana ili Nora asiingie kwenye matatizo kwa maana alijua baba yake ni nani. Lengo la Nora kuwa hapo lilikuwa wazi; kuwasaidia tu kuwapata maadui, lakini kwenye suala la kuwafuata maadui alipaswa kumweka Nora pembeni. Luteni Michael akamhakikishia kwamba Nora angekuwa salama kwa sababu hata leo alimwacha nyuma kabla ya kwenda kwa Oscar, kwa kuwa alijua umuhimu wake. Akamshukuru kwa uelewa wake, naye Kanali Oswald akaondoka hatimaye.
★★★
Lexi na Mensah walikuwa wamefanikiwa kutoka eneo lile na kuondoka jijini hapo haraka sana. Sehemu waliyokuwa wakielekea haikuwa nyingine ila kule "chini," mafichoni kwa timu yao nzima. Victor pia alijiunga nao njiani, kwa sababu upande wa jiji la Dar es Salaam alikokuwa ilikuwa ni mbali, na ndiyo sababu hakuwahi kufika kule Oscar alipokuwa kama alivyowahi Mensah. Walikuwa kimya tu kwa masaa kadhaa wakiwa mwendoni mpaka wanafika kule. Tayari taarifa za kifo cha Oscar zilifikia screen za Torres, ambaye alihuzunika sana. LaKeisha na Kevin waliachwa na simanzi kuu pia kwa kumpoteza mwenzao.
Baada ya Lexi na wengine kufika huko, LaKeisha alimpokea Lexi kwa kumbatio huku akilia sana. Wanaume walikaa tu pembeni wakiwa kimya, bila kutazamana hata kidogo. Lexi alikuwa anatokwa na machozi bila kutoa sauti yoyote, naye akaelekea sehemu yenye chumba pamoja na Lakeisha ili kumtuliza. Alijitahidi kumbembeleza huku naye akiumia sana moyoni. Kulikuwa na hali fulani ya utengano wa kihisia ndani ya kundi hili kwa sababu ya kifo cha mwenzao, na muda ukasonga wakiendelea kuwa hapo bila kufanya lolote zaidi ya kusikitika sana.
★★
Ilifika asubuhi, na boss wao, yaani Kendrick Jabari, akawa amefika huko pia. Aliwakuta vijana wake wakiwa wameketi kwenye chumba cha pamoja, na baada ya LaKeisha kumwona akamfata na kumkumbatia huku analia. Kendrick alikuwa na uso ulioonyesha utulivu tu, naye akambembeleza mwanamke huyo na kwenda kuketi pamoja naye.
Wote walikuwa wamevaa T-shirt nyeusi, isipokuwa Kendrick, aliyefika akiwa amevaa suti yenye rangi ya kijivu. Akaomba aelezewe kila kitu, naye Mensah akamsimulia aliyojionea. Torres pia akaongea, na mwanaume huyo akaeleza mambo yote yaliyotokea kwa upande wake, akisema ni kutokuwa kwake makini ndiyo kulisababisha mambo yote hayo kutokea. Akamwomba Kendrick ampe adhabu kwa sababu hiyo, naye Mensah, Kevin, LaKeisha pamoja na Victor wakasema hivyo hivyo pia kwa kuwa waliona ni kama na wao hawakuwa makini vya kutosha.
Kendrick akamwangalia Lexi. Alikuwa amekaa tu kimya bila kumtazama, huku akipigapiga kidole chake kimoja juu ya meza, naye Kendrick akasimama na kuanza kuondoka hapo. Wengine wakawa wanamwangalia tu mpaka alipokaribia sehemu ya kutokea, kisha akasema, "Nifate," bila kugeuka kumtazama yeyote kati yao, naye akatoka. Kila mmoja wa vijana hawa akamtazama Lexi, wakielewa Kendrick alimaanisha yeye, naye akanyanyuka na kumfuata Kendrick.
Alifika alipokuwa na kumkuta amesimama tu, hivyo akaenda mpaka karibu na kusimama pembeni yake.
"Ni nani aliyemuua?" Kendrick akauliza.
"Sijajua," Lexi akasema.
"Kivipi? Si ulipigana naye?"
"Alificha sura. Huyu hakuwa askari wala... yaani... alikuwa tofauti...."
Kendrick akashusha pumzi. "Unaonaje? Itakuwa sahihi nikiwapa adhabu hawa?" akauliza.
"Wamekosa nini kwani?" Lexi akauliza pia.
"Kama wangekuwa hawajakosea, wasingeomba adhabu..."
"Itasadia nini? Kumrudisha Oscar?"
Kendrick akamwangalia na kuuliza, "Kwa hiyo unataka nifanye nini?"
"Sitaki ufanye chochote uncle. Nataka tu nimshike huyo mpumbavu aliyemuua mimi mwenyewe..."
"Huyu Nora ameshaanza kuwa tatizo kubwa sana. Tunahitaji kumng'oa," Kendrick akasema.
"Uncle... yule yupo kufanya kazi aliyopewa, kama huyo Michael na wengine tu. Hawakuwa na nia ya kumuua Oscar... aliyemuua ni mtu mwi...."
"Lakini ni kwa sababu yake ndiyo maana wameweza kumfikia!" Kendrick akamwambia kiukali.
Lexi akaangalia chini kwa huzuni. "Umenifundisha kutoongozwa na hisia kwenye kuamua mambo ili nifanye maamuzi yaliyo sahihi. Wakati huu ni mgumu kwetu sote uncle, kwa hiyo nakuomba tafadhali tuliza kwanza akili. Mimi pia nahitaji hilo. Kwa ajili ya Oscar... please uncle..." akasema kwa hisia.
Kendrick akabaki kumtazama tu, kisha akaangalia pembeni tena.
Wawili hawa wakaendelea kusimama hapo, bila kujua kwamba Kevin alikuwa amejibanza umbali mfupi kutokea hapo akiwasikiliza. Jamaa akatoka hapo na kwenda kuketi sehemu ambayo alikuwepo Victor akipata chakula kidogo.
"Vipi? Mbona sura ngumu?" Victor akamuuliza.
"Mimi huwa nashindwa kuelewa, basi tu," Kevin akasema.
"Mpaka leo bado hujaelewa nini?" Victor akauliza.
"Si huyu Lexi... sijui yukoje..."
"Amefanya nini, ongea point basi..."
"Hivi ni kwa nini yeye ndiyo anatuongoza sisi? Mm? Ningetarajia kwa mtu kama Torres au wewe na kipaji chako labda hata ndo' ungekuwa mbele yetu, lakini eti na wewe unapewa maagizo na hako kasichana unakokazidi umri..."
"Kwani wewe... ahah... shida yako ni umri tu, au bado roho inakuuma kwa sababu ulimtokeaga akakupiga chini?"
"Siyo hivyo. Me naona mambo yake hayajakaa sawa. Hapa juzi hao mafala walinishika akanikalisha tu hapa, sa' hivi Oscar ameenda... boss anamwambia tumshughulikie huyo Nora, eti anakataa. Me nakwambia wote humu ndani mtakufa kwa sababu yake," Kevin akasema.
Victor akaweka chakula chini.
"Naomba unisikilize. Tena unisikilize kwa makini sana. Bila huyo msichana sasa hivi usingekuwa hapa, elewa hilo. Ametuongoza vizuri sana tokea wakati ambao haukuwahi fikiri kuna watu kama sisi, vizuri kuliko hata Raisi wa nchi hii anavyodanganya kufanya. Hii kitu ya Oscar.... Kevin, hatukuiona inakuja. Siyo kwamba kwa sababu kuna mambo tunayafanya vizuri hiyo imaanishe sisi ni wakamilifu, NO! Makosa yatatokea tu, upende usipende. Ikiwa boss angekuwa amekupa wewe ndiyo utuongoze sisi, haki ya Mungu nakwambia tungekuwa tunanyea debe sa'hivi, ohooo!" Victor akasema.
Kevin akawa anayasikiliza maneno yake lakini kwa kukerwa.
"Heshimu kilichowekwa, acha kulalamika-lalamika. Lexi akiona hapa inafaa, inafaa. Akiona jambo halifai, ujue kweli halifai. Alikwambia ukae huku, mpaka sasa hivi uko salama. Ungekuwa nje kama Oscar...." Victor akaishia hapo na kumwangalia tu usoni.
Akabeba chakula chake na kujiondokea tu, akimwacha Kevin bado akiwa anaona kama vile mambo yote yaliyotokea yalikuwa ni makosa ya Lexi, na kulipaswa kufanywe jambo fulani ili kurekebisha hayo yote.
★★
Kendrick na Lexi walijiunga na Lakeisha pamoja na Torres, wakijadiliana kuhusu njia ambayo Luteni Michael na ACP Nora walitumia kumpata Oscar. Lexi akawaambia kwamba alimwona mwanaume yule aliyefanya kazi benki kuu pamoja nao, yaani Nathan Masunga, naye Torres akatambua sasa kwamba walimpata Oscar kwa njia hiyo. Akawakumbusha kuwa Oscar alitumia jina bandia la Erick kipindi kile wanajipanga kuiba pesa zile, na alimlipa jamaa ili siku hiyo asiende kazini. Torres akawa anaona sasa kwamba kiukweli ACP Nora alikuwa mwerevu kupita maelezo mpaka kufikiria njia hiyo ili kugundua ukweli, na bado akawa anajilaumu kwa kukosa kuwa makini siku ya jana.
Kendrick akasema kwamba kuanzia sasa mambo yangetakiwa kuwa sawa zaidi. Aliwataka wawe makini hata zaidi ili watimize yale waliyotaka kuyatimiza kwa wakati mwafaka. Baada ya hapo, Kendrick akaondoka huko "chini" ili kurudi Geita haraka.
LaKeisha akaongea na Lexi, akimwambia kilichotokea baina yake na Torres. Lexi akamwambia ilikuwa ni sawa, na ijapokuwa wakati huu walikuwa kwenye huzuni, alifurahia kwa ajili yake. Akampa ushauri kwamba asimwache Torres maana ni mwanaume mzuri sana, kisha naye Lexi akaenda kwa Torres, ambaye alimpatia kifaa kingine cha ufatiliaji, halafu akaondoka sehemu hiyo ya maficho.
Torres alimfanyia vipimo Mensah kuelewa ni njia gani adui yao mpya aliitumia kumpiga bila kutumia nguvu nyingi mpaka mwanaume huyu akaishiwa nguvu kabisa, lakini bado hakuweza kuelewa. Kwa hiyo sasa Mess Makers wakawa na adui mpya asiyefahamika, na pengo kubwa sana kwenye timu yao lililoachwa na kijana Oscar.
★★★★★★★★★★
ITAENDELEA
★★★★★★★★★★
Comments