FOR YOU 3
A Story by Elton Tonny
Familia, Urafiki, Mapenzi, Mahaba, Tamaa, Hila, Usaliti, Unyanyasaji, Uhalifu, Mauaji, Visasi, Vita, Mambo yasiyotazamiwa
R-rated 18+
Enjoy!
★★★★★★★★★★★★★
SEHEMU YA KWANZA
★★★★★★★★★★★★★
MIAKA NANE ILIYOPITA....
Turudi tena mpaka usiku ule ambao familia ya Meja Casmir ilishambuliwa na Luteni Weisiko pamoja na wanajeshi wake wawili. Baada ya Weisiko na Goko kuwaua wazazi wa watoto wale watatu, Casmir na Alice, pamoja na msaidizi wao wa kazi Salome, watoto walikimbilia msituni huku Xander, akiwa ndani ya mwili wa Sandra, akiwa na maumivu tumboni kutokana na kuchanwa kwa kisu, naye Sandra, akiwa ndani ya mwili wa Xander, akihisi maumivu pia kwenye paja lake baada ya kuchunwa na risasi aliyofyatuliwa na Goko.
Kutokana na jinsi watoto walivyokuwa wakikimbia polepole hasa kwa sababu ya Sandra kumshikilia Xander kutokana na mwili wake kuishiwa nguvu kwa sababu ya kisu alichochomwa tumboni, Xander akawaambia wenzake wamwache nyuma ili dada zake wakimbie pamoja. Sandra akawa anakataa, lakini Xander akamshawishi kwa kumwambia ni bora hata kama akifa yeye lakini ndugu zake wawe na nafasi kubwa ya kupona kuliko ikiwa wote watauliwa.
Kwa hiyo akamwambia waelekee upande mmoja, halafu yeye atajitahidi kuelekea upande mwingine akiacha viashiria kwa wanaume wale ili wamfate yeye tu. Sandra akiwa kwenye mwili wa Xander alilia sana. Azra alilia pia mno, nao wote wakamkumbatia ndugu yao, kisha akawasihi wawahi haraka maana alijua Weisiko na mwenzake walikuwa nyuma yao.
Sandra, akiwa kwenye mwili wa pacha wake akaondoka na Azra kuelekea upande mmoja, wakimwacha Xander anajiandaa kuelekea upande mwingine. Alijitahidi kukimbia pamoja na Azra kwa uangalifu ili kuwaepuka maadui, huku Azra naye akijikaza sana kukimbia ingawa alikuwa amechoka. Walikimbia na kukimbia bila ujuzi wowote wa walikokuwa wakielekea, na kwa sababu ya kutotambua uelekeo wao ikawa ni kama wanazunguka msitu tena na kurudia njia ile ile waliyotokea.
Azra akafikia ukomo wa pumzi zake, naye akamwomba "Xander" wapumzike kidogo kwa kuwa hangeweza kuendelea kukimbia. Sandra kwa kuhofia usalama wao, akaamua tu kumbeba mgongoni ili waendelee kukimbia, akitumia vizuri nguvu ya mwili wa kaka yake ili iwafikishe mbali. Kichwani kwake alimuwaza sana Xander, angekuwa kwenye hali gani kwa hizo dakika chache walizotengana.
Wakati akiendelea kukimbia hivyo, akaukwaa mguu wake na kudondoka pamoja na Azra. Bado alihisi maumivu kwenye paja lake, lakini akawa anajitahidi kumnyanyua mdogo wake ili waendelee kukimbia. Azra sasa akasema angeweza tena kukimbia, lakini shida ikawa kwa Sandra. Alihisi mguu wake ukiwa mzito sana, kama vile ulikuwa umeanza kufa ganzi, kwa maana kila alipojaribu kusimama vizuri asingeuhisi vyema, na hilo likasababisha awe anadondoka tu.
Azra akajitahidi kumsaidia ili waondoke pamoja, na ni hapa ndipo wakaanza kusikia sauti za hatua zikija upande wao. Kwa kutambua bila shaka ilikuwa ni adui, wakaendelea kujivuta kwa pamoja ili kumwepuka, lakini Sandra akamwambia Azra wajifiche tu sehemu fulani ili adui yao awapite, kwa kuwa kuendelea kukimbia namna hiyo hakungeleta matokeo mazuri sana.
Kwa hiyo wakaketi kwenye kichaka kimoja ambacho kilikuwa na miiba midogo-midogo, na ingawa iliwachoma lakini wakajikaza tu na kuendelea kutulia. Kutulia huku kulifanya maumivu kwenye paja la Sandra yasikike zaidi, lakini akajitahidi tu kujikaza pia. Hazikupita sekunde nyingi, nao wakamwona mtu fulani akifika hapo kando yao. Kwa haraka wakatambua ilikuwa ni Luteni Weisiko, naye Sandra akambana zaidi Azra kwake ili wasitikisike. Luteni Weisiko akasimama hapo kwa sekunde chache, kama akitathmini watoto walikuwa wameelekea wapi, kisha akaendelea kukimbilia upande mwingine.
Baada ya Sandra na Azra kuona ameondoka, wakajitoa kwenye kichaka hicho, naye Azra akamwambia aliyemwona kama Xander kwamba wangepaswa kurudi nyuma ili kumtafuta "Sandra." Lakini Sandra akasema hata hakujua walikokuwa, hivyo hangejua wapite wapi labda mpaka wasubiri kukuche, lakini Azra akasisitiza kwamba walipaswa kurudi kumsaidia ndugu yao hasa kutokana na jinsi alivyoumia.
Sandra akiwa anafikiria nini cha kufanya, wote wakastushwa na sauti ya Luteni Weisiko ikisema, "Njooni na mimi, nitawapeleka kwa dada yenu."
Wawili hawa walishtuka sana na kutazama upande ambao walimwona Luteni Weisiko akiwa amesimama huku anawaangalia. Hofu ikawajaa sana, naye Sandra akamwambia Azra akimbie haraka. Azra akaanza kukimbia kuelekea upande mmoja, naye Sandra akaanza kuelekea huko huko. Luteni Weisiko akaendelea kusimama hapo hapo na kutabasamu tu, kisha akaikoki bunduki yake na kuanza kuwafata kwa kasi. Ilikuwa ni kama alipenda sana mchezo huu wa paka na panya, na baada ya kuwakimbiza kwa hatua kadhaa, akawaona wakiwa kwa mbele wanakimbia, wakijitahidi kuokoa maisha yao.
Walikuja kufika sehemu ambayo ilikuwa na eneo lenye uwazi kidogo bila kuwa na miti bali majani tu chini, na baada ya Luteni Weisiko kuingia hapo akasimama na kuielekeza bunduki yake kwa Azra, aliyekuwa mbele zaidi, naye akafyatua risasi iliyompata nyuma ya mguu wake wa kushoto. Azra alipiga kelele ya maumivu na kudondoka chini, lakini ni wakati tu amedondoka chini ndiyo akapiga kichwa chake kwa nguvu sana kwenye jiwe dogo na kupoteza fahamu.
Sandra akiwa ndani ya mwili wa Xander alipiga kelele ya kilio baada ya kushtushwa na sauti ya risasi hiyo, naye akaanguka chini akiwa amejikunja kwa woga mwingi. Luteni Weisiko akajisawazisha na kuanza kumwelekea mpaka pale alipokuwa, na alipofika karibu, akamwelekezea bunduki yake kichwani kama anataka kumfyatua kwa risasi.
Sandra akawa anamwangalia huku analia na kuficha uso wake kwa mikono. Weisiko akawa anataka kukivuta kifyatulio cha risasi, lakini akasikia mlio wa risasi nyingine kutokea upande tofauti na huo. Akatazama upande huo wa msitu na kukisia kwamba bila shaka ilikuwa ni Goko ndiye aliyempata pacha wa kike na kummaliza, hivyo akaishusha bunduki yake na kumtazama tu pacha huyu wa kiume.
"Umebaki wewe," Luteni Weisiko akamwambia hivyo "Xander" huku akitabasamu.
"Tafadhali... usiniue... please..." Sandra akawa anaomba kwa sauti tetemeshi.
Luteni Weisiko akachuchumaa na kumtazama kwa ukaribu.
Sandra akawa anajivuta nyuma kwa woga.
"Unajua hapa ni sawa na kama umeshakufa kwa sababu... hata nikisema nikuache, huu msitu una wanyama wakali. Ni bora tu nikusaidie ili wasikutafune..." Weisiko akasema.
Sandra akawa anatikisa kichwa kukataa.
"Cha risasi ni rahisi zaidi kuliko meno. Au unataka kutafunwa? Si bora hivi?" Weisiko akauliza kikejeli.
"Una watoto?" Sandra akauliza.
Luteni Weisiko akabaki tu kumtazama.
"Ikiwa ungekuwa nao... na uko sehemu fulani ukijua kabisa wanapatwa na mambo kama haya yanayotupata sisi... ungefanya nini?" Sandra akauliza.
Luteni Weisiko akainamisha uso wake kama anatafakari jambo fulani. Yeye aliona ni kama Xander ndiyo anamuuliza hivyo, na kiukweli maneno yake yalimgusa kwa kiwango fulani.
"Nitakupa dakika mbili tu za kufanya chochote kile unachotaka kufanya. Baada ya hapo...." Luteni Weisiko akaishia tu hivyo na kusimama.
Sandra akaanza kujivuta kuelekea kule alikoangukia Azra. Akafika mpaka karibu yake na kuanza kumpepesa ili aamke, lakini akawa ametulia tuli tu. Aliposikiliza mapigo yake ya moyo, akatambua kwamba bado alikuwa hai, naye akamgeukia Luteni Weisiko kukuta tayari akiwa amewakaribia.
"Please usiniue... please... I'm begging you..."
Luteni Weisiko akaonekana kutojali kilio cha kijana huyu na kuielekeza bunduki yake kwake kwa mara nyingine. Sandra akajisawazisha na kupiga magoti, akiwa ameviunganisha viganja vyake.
"Usiniue tafadhali. Azra... mdogo wangu ananihitaji. Ana tatizo la upumuaji, ana... ana... ananihitaji... tafadhali...." Sandra akaendelea kuomba.
Maneno haya ya Xander (Sandra) yakamfanya Luteni Weisiko aishushe bunduki yake kidogo. Ni kama alikuwa anatafakari jambo fulani baada ya Xander (Sandra) kusema kwamba mdogo wake alikuwa na tatizo la upumuaji, naye akamwangalia Azra pale chini. Lakini akayakaza meno yake na kumwangalia tena "Xander." Akainyanyua bunduki yake kwa njia yenye uhakika zaidi wakati huu, naye akaikoki tayari kumfyatua risasi.
"Usiniueee... pleeease... please usi... usiniueee..." Sandra akaendelea kumwomba hivyo Luteni Weisiko, naye Weisiko akawa kama anataka kufyatua lakini anasita.
Kutokea kichwani kwake, Sandra akasikia sauti ya pacha wake ikimwita, 'Sandra... Sandra...' na kwa sababu hakujua ilitokea wapi, akatafuta utulivu kidogo ili aweze kumsemesha pacha wake pia.
Luteni Weisiko akawa bado amemwelekezea bunduki, naye akasema, "Nisamehe... hii ni sehemu tu ya kazi yangu."
Sandra akafumba macho yake na kuamua kujaribu kuongea kwa kutumia akili yake pia, akiwa ameshakubaliana na matokeo. Ilikuwa ni muhimu sana kwake pacha wake asikie maneno yake ya mwisho.
'Xander... popote ulipo... jua nakupenda sana pacha wangu... tafafhali pambana usalimike... usisahau hili kamwe... for me...'
Lakini kabla hajamaliza maneno yake, Luteni Weisiko akamfyatua kwa risasi kichwani, naye akaanguka chini karibu kabisa na alipokuwa amedondokea Azra. Luteni Weisiko akakaza meno yake kwa nguvu na kutazama pembeni, akiwa kama mtu aliyefanya jambo hilo kwa shingo upande. Lakini akajikumbusha yeye ni nani, mwanajeshi mtiifu ambaye hakupaswa kuruhusu hisia zimkengeushe kutoka kwenye "mission" aliyopewa, hivyo akajisawazisha akili tu na kuwaangalia tena watoto hao, kisha akaanza kuwasogelea chini hapo. Mkono wake uliokuwa umepigwa kwa risasi bado ulitoa maumivu, lakini akawa anaupuuzia tu.
Alipowakaribia zaidi, akachuchumaa na kumwangalia Azra. Kwa hapo angeweza kuhisi tu kwamba binti huyo bado alikuwa hai, naye akaushika uso wake mweupe ambao ulionekana vyema kwenye giza hilo la msitu. Alimwangalia mno binti huyo mdogo, na kumbukumbu kadhaa za matukio ya kipindi cha nyuma zikamwingia akilini mwake.
Luteni Weisiko alikuwa na mtoto wa kike, ambaye kwa sasa hakuwa hai. Binti yake huyo alikuwa mweupe kufata weupe wa mama yake, ambaye Luteni Weisiko aliachana naye kwa kuwa mwanamke huyo hakupenda tabia za kitemi-temi za mwanaume huyu. Lakini Weisiko alimpenda sana binti yake ingawa hakumpa muda mwingi wa kuwa pamoja naye kama mzazi. Binti yake huyo aliitwa Mary, naye alikuwa na tatizo la upumuaji ambalo liliongezeka sana kufikia wakati alipokuwa na miaka 13; rika kama la Azra tu.
Kipindi fulani Weisiko alipokuwa kazini, binti yake alishikwa na mkazo mbaya sana kwenye mapafu, na mama yake alijaribu kumtafuta Weisiko ili amsaidie kuweza kumpatia matibabu ya haraka, lakini Weisiko alichelewa, na hivyo mtoto huyo akapoteza uhai. Mzazi mwenza alimlaumu sana Weisiko kwa kifo cha bintiye, akisema alikuwa na uwezo mzuri tu wa kumpatia matibabu mapema sana hata nchi za nje, lakini akampuuzia. Ila ukweli ni kwamba Luteni Weisiko alikuwa na deni kubwa wakati huo ambalo alikuwa akilipia fidia mfululizo, ndiyo sababu hakuweza kulipia matibabu ya hali ya juu kwa ajili ya binti yake.
Mwanamke huyo aliyezaa naye alikuwa msusi tu kwenye saluni za wanawake, hivyo hakuwa na kipato cha kutosha na alihangaika kwa muda mrefu na binti yake. Kwa hiyo alimlaumu sana Weisiko kwa kuwa aliona kwamba mwanaume huyo kwa mtoto wao alikuwa baba jina tu. Weisiko pia alijilaumu mno kwa kukosa kumsaidia binti yake, na ndiyo kutokea hapo akaapa kufanya kila alichoweza ili kupata pesa nyingi zaidi kwa sababu aliona jinsi maisha yalivyokuwa na hasara bila kuwa na pesa ya kutosha. Akaanza kujihusisha na masuala haramu ya chini chini ambayo ndiyo mpaka yakapelekea yeye kujiingiza katika visa hivi viovu ili tu apate jambo ambalo aliona ndiyo muhimu zaidi lililobaki kwenye maisha yake: pesa.
Kwa hiyo kumwangalia Azra kulimfanya aone ni kama anamtazama Mary kwa mara nyingine tena. Maneno ya "kaka yake" kwamba Azra alikuwa na tatizo la upumuaji, yalichochea hata zaidi hisia hizo kumwelekea binti huyu, naye akahisi eti ni kama alipaswa "kumsaidia," kana kwamba anapewa nafasi ya pili ya "kumsaidia" mtoto huyu kwa kuwa wa kwake alishindwa. Akili yake ilikuwa imeingiwa na suto kubwa kwa sababu ya mambo maovu aliyofanya, kwa hiyo fikira ya "kumsaidia" mtoto huyu ikaonekana kama njia yake ya kujiaminisha kwamba alikuwa na moyo mzuri.
Akatoa simu maalumu ya kijeshi (walkie talkie) na kupiga kwa Kanali Jacob Rweyemamu ili kumtaarifu kwamba mambo yalikamilika. Baada ya kupokelewa, Luteni Weisiko akasema tu, "Mission Accomplished," kisha akarudisha kifaa hicho mfukoni na kuanza kumnyanyua Azra kwa mkono mmoja. Aliweza kuona jinsi ambavyo damu nyingi zilivuja mguuni kwake, naye akachana sehemu ya nguo ya "Xander" na kumfunga Azra sehemu iliyovimba kwa risasi. Akambeba begani kwake kama vile windo la swala, kisha akaanza kuondoka naye.
Alikwenda taratibu kama vile hakukuwa na tatizo lolote kabisa mpaka akafika kule ambako kulikuwa na nyumba ile alikowaua wazazi wa watoto hawa. Akampeleka Azra mpaka ndani ya gari walilokuja nalo hapo, naye akaanza kumtafuta Goko kwa kifaa kile cha mawasiliano. Alifikiri angemkuta huku tayari kwa sababu alisikia risasi ile iliyofyatuliwa kutokea upande ambao alimwambia aende. Kwa sababu hakuweza kumpata, akaona tu aondoke hapo ili kumpeleka binti huyu kwenye matibabu. Alimwangalia kwa mara nyingine na kuona bado yuko hai, naye akawasha gari na kuondoka hatimaye.
★★★
Akiwa bado mwendoni, Weisiko aliongea na baadhi ya vijana wa kundi lao na kuwaeleza kile yeye na wengine wawili walichofanya usiku huo, naye akawaamuru baadhi kwenda sehemu ile alikotoka ili kuteketeza miili ya wale waliowaua. Akawapa maagizo hususa kabisa kwamba walipaswa kupeleka na miili mingine ya watu waliokufa ili kuichoma kwa moto pamoja na ile ambayo wangeikuta, na walipaswa kumaliza hayo yote kabla ya jua kuchomoza. Akamalizana nao na kuendelea na safari yake, akiwa na lengo la kumpeleka Azra kwenye hospitali ya jeshi. Yaani ilikuwa ni kama akili yake imekufa ganzi kabisa, akifanya mambo kwa njia aliyoona kuwa sahihi, na hakuna kitu chochote ambacho kingemzuia.
Alifika kwenye hospitali ndogo ya jeshi na kupokelewa na baadhi ya vijana ambao alikuwa ameshawapanga. Walimpokea kwa njia yenye umakini ili kuwaficha wengine ambao hawakuwa wa kundi lao kuhusiana na yaliyotokea. Eneo la huku lilikuwa kwenye kambi kubwa sana ya kijeshi ambako wanajeshi wengi waliishi. Kwa hiyo vijana wake hao wakampeleka Azra kwenye chumba cha matibabu, na daktari wa upasuaji (akiwa ni mwanajeshi pia) akafika na kuanza kumhudumia mtoto.
Weisiko aliketi kwenye kitanda cha pembeni ndani ya chumba hicho hicho, akiwa anatolewa risasi mkononi mwake, na hakuna yeyote aliyepaswa kuuliza ni nini kilikuwa kimetokea. Walipaswa kuwapa tiba, halafu waendelee na mambo mengine. Weisiko akawaambia watu wake wamwangalie vizuri sana huyo mtoto, yaani wafanye lolote lile lakini asife, nao wakaendelea kujitahidi kumpa Azra huduma mpaka inafika asubuhi. Walifanikiwa kuitoa risasi mguuni kwake na kumshona, nao wakatibu sehemu ya kichwa chake iliyoumia na kuifungia bendeji. Sasa mtoto akawa anasubiriwa kurejesha fahamu.
Taarifa kumhusu Azra kuwa hapo zilipaswa kuwa za siri sana, ikiwa ni amri kutoka kwa Luteni Weisiko. Lakini alijua kwamba huenda asingefanikiwa kuficha hili kwa wakuu wengine kwa muda mrefu sana, hivyo asubuhi hiyo akaamua kumwambia Kanali Jacob Rweyemamu kila kitu akichofanya. Kanali Jacob kiukweli alimshangaa na kuuliza ikiwa akili yake ilikuwa imekongoroka au alikuwa anataka kuwaletea matatizo mapema. Lakini Luteni Weisiko akamwambia kuna hali ilimsukuma kumsaidia mtoto huyu, hasa kwa sababu alimkumbusha kuhusu binti yake aliyeshindwa kumwokoa.
Kanali Jacob akamwambia kwamba hilo halikujalisha hata kidogo. Ikiwa msichana huyo angeamka na kusema kila jambo lililotokea basi mambo kwao yangeharibika. Akamuuliza Luteni Weisiko angewezaje kuzuia hilo, ndipo Weisiko akamwambia kwamba alipanga KUMSAHAULISHA Azra mambo yote yaliyotokea. Yaani alitaka mtoto huyo apoteze kumbukumbu ya mambo yaliyotokea, lakini pia kuhusu yeye ni nani KABISA.
Kanali Jacob alipouliza nia yake ya kufanya hayo kiukweli ilikuwa nini, Weisiko akasema alitaka kumfanya Azra kuwa kama "binti yake," kwa sababu kila kitu kumhusu huyo mtoto kilimkumbusha kuhusu Mary. Akamwomba sana Kanali Jacob amkubalie kuhusiana na hili, akisema ana njia ya kufanya hivyo, na hakuna jambo lolote ambalo lingeharibika kwa kuwa amehakikisha mipango yao yote imekwenda "salama."
Pamoja na kwamba Kanali Jacob aliona suala hili kuwa upuuzi wa hali ya juu, akamkubalia tu, naye akamwambia angetumia uchochezi wake kuhakikisha Azra anaendelea kuwa siri hapo kwenye hiyo hospitali. Lakini akamweka wazi kwamba Azra kuendelea kuwa hai nchini humu hata kama asingekumbuka lolote bado kungekuwa hatari kwao, hivyo akapendekeza kwamba walipaswa kumhamisha na kumpeleka nje ya nchi. Akiwa nje ya nchi kwa kipindi kirefu ingesaidia kumfanya asahaulike kabisa hasa kwa sababu watu wangefikiri ameshakufa kama tu watu wa familia yake, naye Weisiko akakubaliana na hilo.
Lakini kwanza wangehitaji kumalizia sehemu muhimu ya mipango yao iliyobaki, yaani, kuwaondoa Jenerali Pingu Senganya na Luteni Jenerali Geneya Oyayu, ndiyo wangeanza harakati za kumsafirisha Azra.
★★★
Baada ya wiki moja hivi kupita, Azra alirejesha fahamu zake. Alijikuta akiwa ndani ya chumba cheupe, kilichokuwa na mwonekano kama wa vyumba vya hospitali lakini cheupe kupita maelezo. Alikuwa amewekewa 'drip' kwenye mishipa, na aliweza kuhisi jinsi ilivyokuwa ngumu kunyanyua baadhi ya sehemu zake za mwili. Alikuwa akijiuliza alifikaje humo, na kitu chenye kumhofisha hata zaidi ni kwamba hakuwa na kumbukumbu yoyote ya mambo yaliyompata mpaka kufika sehemu hii. Alijaribu na kujaribu kuvuta taswira ya vitu vingi kuhusu yeye, lakini ilikuwa ni kama kichwa chake kilikuwa tupu kabisa.
Hali hii ya kutojielewa ilimfanya aogope sana, hasa kwa sababu alikuwa binti mdogo mno. Akaanza kujaribu kunyanyuka, lakini akashindwa. Akaanza kulia sana, kwa sauti ya chini, na ndipo akaingia mtu aliyemwona kama mwanaume wa kawaida tu. Kwa sababu hakumtambua, mwanzoni alionyesha kuogopa, lakini mwanaume huyo akaanza kumtuliza kwa kumwambia yeye alikuwa ni baba yake. Huyu alikuwa ni Luteni Weisiko.
Akaanza kumdanganya Azra kwa maneno mazuri sana na kumfanya atulie. Akamdanganya kwa kumwambia kwamba jina lake lilikuwa ni Mary. Alimweleza kwamba alipatwa na ajali mbaya sana na ndiyo maana alikuwa kwenye hospitali hiyo kimatibabu. Akasema kwenye hiyo ajali waliwapoteza mama yake na ndugu zake wengine, kwa hiyo walikuwa wamebaki peke yao tu. Azra hangeweza kukumbuka chochote wakati huu kwa sababu ndani ya wiki hiyo tayari Luteni Weisiko alikuwa amefanya ule mpango wake wa kuipoteza kumbukumbu ya binti kwa kutumia madawa fulani. Kwa hiyo yeye kuwa hapo peke yake na kuonyesha anamjali sana Azra, kukafanya binti amwone kuwa mtu wa kuaminika na wa karibu zaidi kwake, hivyo kujihisi salama.
Weisiko akaendelea kukaa na Azra hapo kwa muda mrefu, akimwambia kwamba angempeleka nje ya nchi apate matibabu bora zaidi ili apone haraka. Azra hakuweza kusema lolote lile kwa kipindi hiki. Muda wote alikuwa kimya tu, na akiitikia mambo machache kutoka kwa Luteni Weisiko kwa kutumia ishara. Hata wakati ambapo watu wengine kama wauguzi wangeingia, angeonyesha kuwahofia na kujificha kwa Weisiko, naye angemtuliza. Mambo yote mabaya yaliyompata kwa sababu ya mwanaume huyu yakawa yametoweka kwake, na sasa ikawa kama vile huyu ndiyo mkombozi wake.
Siku kadhaa zilizofuata, Luteni Weisiko, kwa msaada wa Kanali Jacob, akawa amefanya mipango tayari ili kumtoa Azra nchini huku na kumpeleka nchini India. Kanali Jacob alijuana na watu kule ambao wangeweza kumhifadhi binti huyo sehemu ya mbali kwa muda mrefu, naye Weisiko akamhakikishia Azra kwamba angekwenda huko pia baada ya kumaliza kazi fulani huku ili wawe pamoja, kwa kuwa Azra angetangulia. Binti bado hakujihisi usalama mikononi mwa watu wengine, hivyo kwenda na hawa wageni ndiyo ilimfanya aogope hata zaidi. Lakini Weisiko alikuwa amemwambia asiogope, kwa sababu alipaswa kujitahidi kuwa imara zaidi kwa ajili ya "baba yake" ili waje kuwa pamoja.
Kwa hiyo binti akapaa kuelekea kwenye himaya mpya kabisa kwenye maisha yake, akiyaacha maisha ya zamani na kwenda kuanza mapya kabisa.
★★★
Mwanaume aliyekuwa amemchukua Azra na kumpeleka India aliitwa Vivek Nambiar. Huyu alikuwa ni mshiriki mkubwa kutoka kwenye shirika kubwa la kimisaada kutokea India, ambalo lilikuwa na sehemu kubwa pia nchini Tanzania kwa miaka mingi. Lakini kama vile Makamu wa Raisi Paul Mdeme na Kanali Jacob tu, mwanaume huyo alikuwa ni mfisadi wa hali ya juu, akitumia njia mbaya kujipatia mali huku akijifanya mwema kwa kujihusisha na utoaji wa misaada.
Kikundi cha watu wa jamii yao kilikuwa nchini Tanzania, na ingawa wengi walifanya mambo mengi kama kusaidia katika sekta za elimu, afya, na mahitaji mbalimbali kama maji, bado watu kama Nambiar walifanya uovu usioonekana kwa njia ya moja kwa moja kupitia shughuli hizo hizo. Kwa hiyo lengo la Kanali Jacob Rweyemamu la kumpeleka Azra mafichoni lakini kwa mwanaume huyo kihususa, ilikuwa ni ili amjenge kuwa aina ya mtu ambaye angekuja kuwa msaada katika mipango yao ya baadaye.
Sehemu ambayo Azra alipelekwa ilikuwa kwenye eneo lililojulikana kama Kerala, lakini ilikuwa ndani sana kwenye milima na misitu. Huko kulikuwa na majengo ya kale ambayo yalionwa kama mahekalu, na yalitunzwa kisiri sana kwa muda mrefu. Nambiar alijuana na baadhi ya watu wa huko, ambao walikuwa na tamaduni zile za ndani sana. Mara nyingi walipeleka watu fulani huko ili kuwatengeneza kwa njia mbalimbali kuendana na viwango vyao kiakili na kimwili, lakini hasa watoto wadogo. Wangefundishwa tamaduni za hapa na pale, kisha baadaye wangekuja kutumiwa katika masuala mbalimbali kijamii ili kuonyesha tamaduni hizo, au watu hao waliowatunza kupata malipo ya hali ya juu kutoka kwa watu waliowapeleka watoto hao huko.
Kulikuwa na mafunzo ya aina mbalimbali hasa kwa ajili ya maonyesho, muziki, kupigana, na kujihami, na baada ya Azra kukaa huko kwa kipindi cha mwaka mzima, mwanamke mmoja mzee aliyeitwa Madhava Gopinath, ambaye alikuwa mmoja wa walimu huko, aliona kitu fulani ndani ya Azra ambacho kilimwambia kwamba binti huyo angeweza kujifunza mtindo fulani wa kupigana uliokuwa nadra sana kwa wengine kufundishwa.
Mtindo huo ulifundishwa karne na karne nyingi zilizopita, lakini ulikuwa ni mtindo hatari sana endapo ungetumiwa vibaya. Hivyo kwa muda mrefu uliacha kufundishwa, na hata wengi walidhani haukuwahi kuwepo. Ni mtindo uliohitaji kiwango cha juu cha imani kutoka kwa mwalimu ili amfundishe mwanafunzi ambaye alionekana kuwa na utu unaofaa ili kutoutumia vibaya. Na mwanamke huyo akaona jambo hilo kwa Azra.
Kwa muda wote ambao Azra aliishi huko, hakuwa akiongea. Mwanzoni alikuwa akijitenga lakini baada ya muda akawa akichangamana na wengine na kufuata maagizo yote aliyopewa, lakini bado alikuwa haongei kwa mdomo. Mwanamke huyo mzee alianza kujenga ukaribu naye zaidi na hivyo kumwelewa vizuri hata zaidi, kwa hiyo baada ya muda alianza kumfundisha njia hiyo pekee ya kupigana na kujihami. Hii haikuwa kati ya mitindo ambayo Kanali Jacob na Weisiko walitazamia Azra kufundishwa, kwa hiyo ikawa ni nyongeza ya siri kwenye mafunzo yake.
Mwanamke huyo alimfundisha mambo mengi sana, na Azra akampenda kama bibi yake. Weisiko alikuwa na kawaida ya kwenda India ili kutumia muda pamoja na "binti yake," na kwa kipindi cha miaka michache ambayo Azra aliendelea kuishi India, alipata aina fulani mpya ya furaha na kujihisi huru na salama. Lakini hilo lisingechelewa kuharibiwa.
★★★
Baada ya Azra kuwa ameishi India kwa miaka zaidi ya saba, Weisiko, sasa akiwa ni Luteni Jenerali, alikwenda na kumchukua kutoka huko ili kumrudisha nchini. Sasa akiwa ni mwanamke mdogo, aliyekuwa na sura nzuri na mwonekano wenye kuvutia, alirudi kwenye nchi yake ambayo hakuwa na kumbukumbu ya mambo mengi kuihusu. Hii ilikuwa ni kwa sababu kwa kipindi chote alichoishi India alikuwa akipewa dawa kupitia Weisiko ambazo alifikirishwa zilikuwa zinamsaidia kiafya, lakini ndiyo zilikuwa zinafanya asikumbuke maisha yake ya zamani. Angalau wakati huu aliweza kuzungumza tena, na alijua lugha tatu; Kiingereza, Kihindi, na Kiswahili, ingawa hakuzungumza Kiswahili kabisa.
Luteni Jenerali Weisiko alimpeleka binti yake huyu kwenye makao yake mapya, ambako ilikuwa ni kwenye moja kati ya nyumba za kifahari za Weisiko. Hii ingekuwa nyumba ya Azra pekee, naye alifurahia sana kuona kwamba "baba yake" alikuwa amempatia zawadi nzuri kama hiyo kwenye siku yake ya kwanza nchini humu. Alitarajia kwa hamu sana kuanza kukutana na watu wengine na hata kujenga marafiki, lakini matarajio yake yakazimwa baada ya Weisiko kumwambia kwamba asingeweza kwenda sehemu yoyote ile na kuchangamana na watu isipokuwa mpaka amwambie kufanya hivyo.
Kwa kutoelewa sababu, Azra aliuliza ni kwa nini, na ndiyo hapa Weisiko akaanza kuijaza akili yake kwa uwongo mwingi sana kuhusiana na maisha yake ya nyuma. Alimwambia sababu iliyofanya mpaka akashindwa kukumbuka mambo ya nyuma ni kutokana na ile "ajali" iliyompata, lakini kuna watu ambao waliisababisha ajali hiyo na hivyo kuharibu maisha yao wakiwa familia. Alimwambia kuwa watu kama hao wangetaka kumdhuru endapo wangejua aliokoka, na ndiyo sababu alimhamisha kutoka huku na kumpeleka Kerala. Akamwambia mafunzo aliyopokea kule yalikuwa ili kumsaidia awe imara, lakini pia endapo maadui wao wangewazingua basi amsaidie kuwafutilia mbali.
Azra alichanganywa sana mwanzoni. Alikuwa amefundishwa kutumia vipawa vyake KUJIHAMI na siyo KUUMIZA mtu, lakini Weisiko alichokuwa anamwambia ilikuwa kwamba endapo angemwomba amshughulikie mtu na kumwondoa kabisa, basi atii. Weisiko alijiweka kwenye upande ulioonekana kuwa mwema, akisema hangemwomba kamwe aue mtu asiyekuwa na hatia, bali wale tu ambao walifanya mambo mabaya kupitiliza. Akamwambia ndiyo sababu alihitaji kukaa kwa siri ili kulinda utambulisho wake. Kwa sababu Azra alimheshimu kama "baba yake" aliafikiana na yale aliyokuwa amemwambia, ijapokuwa moyoni mwake hakuhisi amani.
Kwa hiyo baada ya muda fulani kupita akiwa nchini, Azra aliendelea kukaa mwenyewe, na maisha kwake yalikuwa mazuri na ya hali ya juu kutokana na vitu alivyopewa na Weisiko. Hakuwa tu mtu wa kukaa ndani ya nyumba asubuhi mpaka asubuhi, kwa sababu mara kwa mara alitoka na kwenda kutembea sehemu mbalimbali akiwa mwenyewe, lakini kwa umakini wa hali ya juu. Aliwakumbuka sana baadhi ya watu waliokuwa kama marafiki kwake kule India, na hata mara kwa mara angehisi uhitaji wa kujenga marafiki huku, lakini Weisiko aliendelea kuwa karibu naye kama "baba" ili kutomfanya ahisi upweke.
Ndipo baada ya siku kadhaa kupita baada ya tukio la wizi wa trilioni 20 kwenye benki kuu, Luteni Jenerali Weisiko alikuja kwake na kumwambia kuwa angempa "mission" mpya iliyomhitaji kuwakamata watu wa kundi la Mess Makers na kuwaua. Azra alihofia kwamba huenda asingeweza kutimiza aliyotaka "baba yake," lakini Weisiko akamwambia hakupaswa kuogopa. Alimwambia njia walikuwa wameshamtengenezea, hivyo yeye angepaswa kufanya vitendo tu na kujiondoa sehemu za tukio haraka bila kutambulika. Alitumia kigezo cha kwamba Mess Makers waliumiza na kuua watu wengi tokea walipolipua mabomu kwenye majengo yale, na bado walikuwa wakiendelea kuisumbua serikali, hivyo msaada wake wa siri ungethaminiwa sana.
Azra alikuwa amefunzwa kuwa makini sana, hivyo aliuliza kwa kina mambo aliyohitaji kufanya, ikiwa labda angeshambuliwa na mtu ambaye hakutakiwa kumuumiza, naye Weisiko akatoa kibali cha kuua tu. Alimwambia ilikuwa ni muhimu kwake kufanikiwa katika yote aliyotakiwa kufanya, kwa sababu Raisi alikuwa ameiharibu nchi sana. Ijapokuwa mwanzoni Weisiko alimshawishi kwa kusema anafanya hayo kama njia ya kuwasaidia watu, Azra alikuwa na akili kutambua kwamba kwa jambo hili Weisiko alikuwa anamtumia kama silaha yake maalum, lakini akaacha iwe hivyo tu ili kumridhisha "baba yake" huyo.
Kazi ya kwanza katika mishe hiyo ilikuwa ni kuiweka timu ya Luteni Michael na ACP Nora karibu na macho yake, ili hatimaye aweze kuwafikia Mess Makers. Haikuwa rahisi kwake hata kidogo mara ya kwanza kabisa alipolazimika kuwaua wanajeshi wale watatu, Vedastus, Omari, na Mishashi, pamoja na Oscar Amari wa Mess Makers.
Usiku huo alipotoka kwenye mauaji hayo aliyoyafanya kwa mikono yake mwenyewe, alikwenda sehemu ya mbali na kuanza kulia sana. Alilia mno, kwa kuwa ndiyo ilikuwa mara yake ya kwanza kuondoa uhai wa wanadamu wenzake. Tokea alipopelekwa India, Azra alikuwa mwenye uhitaji wa kujua ni nini lililokuwa kusudi la maisha yake, na sasa ikawa ni kama limefunuliwa wazi mbele yake. Akaamua tu kuliishi sasa, kwa kuwa hicho ndiyo kitu alichotengenezwa kuwa; muuaji.
Weisiko alimmwagia sifa baada ya matokeo ya kwanza ya kile alichofanya, akifikiri kwamba Azra alifurahia sana, lakini kiukweli alikuwa amembomoa kupita maelezo. Furaha aliyokuwa amekuja nayo nchini ilitoweka kuanzia usiku huo alipowaua wanaume wale, na moyo wake ukaanza kugeuka kuwa mgumu zaidi kwa sababu ya hisia za kujichukia. Hakuwekwa wazi kuhusu mambo ambayo Mdeme alikuwa amefanya pamoja na kundi lake kwa muda mrefu, akifikirishwa kwamba yeye yuko upande sahihi kwa sababu ya uwongo ambao "baba yake" alikuwa akiilisha akili yake.
Kwa hiyo kutokea hapo angeendelea kutulia mpaka akiambiwa cha kufanya na Weisiko, naye angetekeleza aliyoambiwa ili tu kumfurahisha, mpaka wakati ambao aliagizwa kumuua Salim Khan....
★★★★
WAKATI ULIOPO....
Siku hiyo ambayo Salim Khan alinyongwa kwenye lifti kikatili sana, Azra alipatwa na jambo fulani ambalo liliisumbua akili yake baada ya kufanya mauaji hayo. Wakati akiwa anapigana na mmoja wa Mess Makers, yaani Lexi, alishindwa kuelewa ni kwa nini mwanamke huyo alijifichua kwake, halafu akaanza kumwita kwa jina la "Azra." Aliendelea kupigana naye, huku Lexi akijitahidi kumwambia aache, lakini Azra hakusikiliza na kufanikiwa kumpiga kwa mtindo wake uliommaliza nguvu Lexi mikononi.
Azra aliposhika kisu na kumfata Lexi akiwa na nia ya kuikata shingo yake, mkono wake ukasita baada ya akili yake kuanza kumwonyesha picha fulani ya mwanamke huyu, kama vile aliwahi kumwona kipindi cha nyuma. Alishindwa kuelewa hiyo ilikuwa ni kwa nini, lakini hisia aliyoipata ilimfanya ahisi ni kama anamfahamu, tena vizuri sana. Akashindwa hata kupitisha kisu kwenye shingo yake kutokana na kuchanganywa na hali hiyo, na ndipo wenzake na Lexi wakafika hapo.
Kwa sababu ya kutotarajia, Azra alishtuka na kuwa kama amepoteza umakini wake, na wakati Mensah alipomwelekezea bastola, akashangaa sana baada ya Lexi kumkinga na kupigwa yeye badala yake. Hapa ni kama umakini ndiyo ukamrudia, naye akatoka eneo hilo upesi na kukimbia kwa kasi yote. Akiwa anakimbia alisikia vizuri sana jinsi mwanamke yule aliyekuwa anakaribia kumchinja alipomwambia mwenzake kwamba asimpige (Azra) risasi, naye Azra akafanikiwa kukimbilia upande mwingine wa uwanja huo na kujificha pembeni ya ukuta; pakiwa na giza.
Maswali mengi sana yalipita kwenye kichwa chake. Mwanamke huyo alikuwa ni nani? Na kwa nini alimkinga asipigwe na risasi? Ni kwa nini alimwita kwa jina ambalo hakuwa na utambuzi wowote kulihusu? Na jambo la muhimu hata zaidi, ni kwa nini yeye Azra alishindwa kumuua alipopata nafasi rahisi zaidi? Kwa kukosa majibu sahihi na kufikiria hali aliyokuwa ndani yake, akaamua tu kuondoka eneo hilo haraka.
★★★★★★★★★
ITAENDELEA
★★★★★★★★★
Comments