Reader Settings

Yulia aliishia kumwangalia Hamza na mwonekano wa macho yasiokuwa na furaha.

“Una uhakika ulikopi   hizo taarifa kwenye tarakishi yake?”

“Ndio”

Hamza alikuwa na uhakika , ingawa hakuwa mtaalamu wa masuala ya  kompyuta, lakini kukopi taarifa halikuwa tatizo kwake.

“Kama ni hivyo basi Saidi hakuwahi kuweka taarifa za tafiti zake kwenye tarakishi”

“Unataka kusema  kwamba  taarifa nilizokopi kwenye tarakishi hazikuwa  teknolojia ya  kutengeneza maroboti ya kibailojia?”

Hamza alionekana kushangaa , mwanzoni  alijua Yulia atakuwa amezifanyia kazi taarifa  hizo na kuja kwake hapo angepata  majibu  kumbe zilikuwa sio sahihi.

Kusikia taarifa hio , Hamza hakujua  awe na furaha au  awe na wasiwasi , alihisi  furaha kwasababu  Yulia kukosa taarifa hio  ingemzuia kufanya mambo ya hatari, lakini kilichompa  wasiwasi ni kwamba  kama Saidi atarudi na hakuna taarifa zozote juu ya  tafiti hizo  ingekuwa ngumu zaidi kudili na Saidi.

“Huyu  Saidi niseme tu  , anao uwezo. Hii inamaanisha  taarifa zote amezikariri , ili  ziwe salama zaidi”

“Usimuwazie sana , una  Earth Axis tayari , huna haja ya kuwazia teknolojia za Saidi . ngoja  kwanza nikutambulishe. Huyu ni Braza wangu , jina lake anaitwa  Zade Maduli. Tafuta namna ya kumpa nafasi ili aweze kukupa ulinzi masaa ishirini na nne , itakuwa vizuri zaidi akiwa undercover”Aliongea Hamza na kumfanya  Yulia kumwangalia Zade.

“Kwanini ghafla tu ukaamua kuniandalia bodigadi, tayari yupo Bertha , ijapokuwa simpendi , lakini huyu mtu wako ana nguvu kumzidi Bertha kweli?”

“Sio mtu wangu , jina lake anaitwa Zade na anayo kila sifa”

“Mh! Kwahio unawaswasi na usalama wangu sana ndio maana ukaniandalia mtu wa kunilinda?”

“Wewe ni mpenzi wangu , hivyo  ni jukumu langu kuhakikisha usalama wako. Nimeingia katika mgogoro na  waumini wa Sinagogu  na nguvu yao imegeuka kuwa kubwa kuliko nilivyofikiria. Ili kujilinda mwenyewe  napaswa pia kulinda watu wanaonizunguka”

Yulia mara baada ya kusikia maelezo mafupi ya Hamza alionekana  kuelewa.

“Kama ni hivyo basi ngoja nitamuona , kwanzia sasa utakuwa unanifuata pamoja na Bertha , lakini hakikisha  usiigize anachokifanya Bertha”

“Madam , jina langu naitwa  Zade”Aliongea Yule ninja kwa ukauzu mara baada ya kuhisi dharau kutoka kwa Yulia.

Hamza mara baada ya  kumpa maelezo machache Zade alipanga kuondoka , alipanga kuonana na Eliza pamoja na  Prisila ili kuwapatia zawadi zao.

“Hamza kuna harambee na mnada  kesho kutwa , vipi  na wewe unaenda?”

“Harambee na mnada ,  ni   wa nini?”

“Kwani Regina hajakuambia?”

“Mke wangu hajaongea chochote ,  kwani vipi?” Yulia mara baada ya kusikia hivyo alionekana kupatwa na hali flani hivi kama mtu alielewa jambo na kisha akaongea.

“Nadhani alifanya makusudi kutokukuambia..”Aliongea na kuanza kumwambia kuhusu Mnada huo  pamoja na Harambee.Na Hamza mara baada ya kusikiliza maelezo ya Yulia hatimae alionekana kuelewa.

Kumbe  kila mwisho wa mwaka wafanyabiashara wakubwa ndani ya jiji la Dar es salaam , hukusanyika pamoja kuchangishana  hela pamoja  na kufanya mnada   ambao ungesaidia katika   misaada ya watu wasiojiweza. Mnada huo pamoja na Harambee hufanyika kila mwisho wa mwaka mara moja tu.

Kushiriki katika mnada huo ni  moja ya sehemu ya kujijengea taswira na heshima kwa jamii. Ni mnada ambao mara nyingi  huhusisha kupiga mnada wa vitu vya  watu wa kawaida, iwe ni wasanii  au wabunifu , huleta bidhaa na kisha hupigwa mnada  kununuliwa na matajiri.

Vitu hivyo  havina thamani sana kwa matajiri hao , mara nyingi  ni kama  utaratibu tu au namna ya kutoa msaada ,  lakini malengo makubwa pia ni kuhimiza  wabunifu na wasanii kuongeza juhudi pia , kuliko ile kutoa hela moja kwa moja bila ya  kufanya kazi. Hivyo  ni mnada ambao ni maarufu mno.

“Regina anashiriki pia kila mwaka ,  tena kawaida kwasababu nyie ni wanandoa unapaswa kushiriki nae , lakini kwasababu  hajakuambia labda hataki kuongozana na wewe  au hataki nikuone”Aliongea Yulia  huku akicheka.

“Sio  lazima iwe kweli , pengine hajapata tu muda wa kuniambia”

“Basi kama hatokuambia  , unaonaje tukishiriki pamoja?”Aliongea huku akiwa na mwonekano wa kichokozi.

“Huna haja ya kunichokoza , siwezi kuthubutu”

“Mhmh , nilijua huwezi kuthubutu”Aliongea Yulia huku akimwangalia Hamza na macho yaliojaa masikitiko

“Unaweza kwenda, tutawasiliana  kukiwa na lolote ,  nataka kwanza nidili na huyu Yasin”

Hamza hata yeye pia alitamani kumfurahisha Yulia , lakini ingekuwa ngumu  kwenda nae yeye na kisha akamuacha  Regina , ingekuwa ni ushenzi wa hali ya juu sana.

Hamza muda wote wa mchana aliutumia kugawa zawadi ,  alianza  kumpelekea  Prisila ambae alifurahi kumuona na pia kupewa zawadi , isitoshe  ilikuwa zawadi ya pili kutoka kwa Hamza. Ya kwanza ilikuwa ni gauni ambalo hakuwahi kuwazia kulinunua.

Hamza mara baada ya kufika kwa  Eliza  na kumpelekea zawadi  , mrembo huyo alifurahi , sio kwasababu  ya  thamani kubwa ya zawadi hizo bali Hamza aliwakumbuka ndugu wazazi na ndugu zake  kuwanunulia zawadi.

Eliza alimwabia Hamza ndugu zake  wangekuja Dar  kwa ajili ya sherehe ya Christmas na kama atakuwa na muda anakaribishwa.

“Nitaangalia itakavyokuwa , ijapokuwa naweza kuwa bize sana siku hio , ila nitaangalia namna ya kupata chakula pamoja”

Ukweli ni kwamba ndugu wa  Eliza walitamani sana kumuona  Hamza , hio yote ni kutokana  na msaada mkubwa alio wapatia , walikuwa wakijua Hamza ana  mke hivyo waliona isingekuwa  sahihi kumwambia Eliza ampeleke  Iringa na badala yake  waliona  wao ndio waje wapate nafasi ya kumuona.

Kati ya wanawake wote Hamza hakupanga kupelekea zawadi  ni Irene, kwasababu hisia zake kwa mwanamke huyo bado  hazikuwa zimeeleweka bayana. Mara baada ya kufika nyumbani  alimpigia simu na kuongea nae na simu na kisha kukubaliana kuonana  siku inayofuata. Mara baada ya kukata simu alijua Regina alisharudi kazini hivyo alitoka chumbani na kushuka chini.

Wakati anashuka , aliweza kumsikia Regina akiongea na Shangazi  kwa furaha  jikoni.

Regina alikuwa hata  hajafika chumbani kwake na kubadilisha na alionekana  akiongea  mfululizo.

“Shangazi , nishaanza kupatwa na msisimko kabisa , kumbe kuvuna nishati  kunamfanya mtu kujisikia vizuri hivi , yaani nahisi  mwili wangu wote ni kama umeshikwa na hali ya ubaridii na  naweza  kusikia pumzi zangu”

Shangazi aliekuwa bize kuandaa chakula aliendelea kumsikiliza Regina na  tabasamu  tu.

“Ni hatua nzuri , hapo unachukuliwa  umeingia rasmi katika hatua ya  nusu mzunguko. Nadhani  nafsi ya bibi yako inakuangalia na kukuongoza”Aliongea Shangazi akiwa na furaha kubwa.

Shangazi pia ni mtu wa  Bondeni , kama  Regina akiweza  kuvuna nishati na kupanda  levo , ingekuwa rahisi kwao  kurudi kwenye asili yao na kupokelewa.

“Wife  ndio kwanza  upo kwenye  daraja  la nusu mzunguko . Safari iliopo mbele yako ni ndefu mno, huna haja ya kufurahi namna hio”Aliongea Hamza alieegamia mlango wa jikoni.

“Unadhani kila mtu ana kipaji kama wewe! Sijawahi kuwazia katika maisha yangu nitakuja kuhisi  hivi , watu wenye nishati za mbingu na ardhi niliwaona kama watu waliopatwa na bahati . Sasa na mimi nimepanda levo kwanini  nisifurahi ?”

“Haha , Regina , umejaaliwa akili nyingi , nina uhakika ukiendeleza juhudi utakuwa mtaalamu hapo baadae. Kuhusu  mwisho utakaofikia ni ngumu kutabiria  kwasasa”Aliongea  Shangazi.

Hamza alisogea na kumshika Regina mkono na kupima  msukumo wa damu na macho yake yalionyesha mshangao , ilionekana ni kweli ,  nguvu ya  msukumo wa damu   ilionekana kuwa mara mbili  na mwanzo.

“Hili andiko linaonekana kuwa na  nguvu kubwa kweli , yaani ndio kwanza upo levo ya nusu mzunguko  lakini mzunguko wako wa damu umeimarika kiasi hiki?”

“Ni urithi wa babu na bibi walioniachia , halafu sasa hivi baada ya kujihisi hivi nimegundua naweza kufanya kitu  cha kimaajabu”

“Kitu cha kimaajabu , unamaanisha nini?”Aliongea Hamza  kwa mshangao na haikuwa kwake tu hata kwa  Shangazi pia.

Regina alichukua  glasi na kisha alimimina maji ya moto kwenye ile  glasi  na kisha  akaishikilia kwa nguvu , ndani ya  sekunde chache tu yale maji yalianza kupoa kwa kasi ya ajabu sana na kuwa ya  baridi  kiasi cha kuelekea kushikwa na ukungu wa ubaridi.

“Mnaonaje haya maajabu , kipindi cha jua kali naweza tu nunua  Strawberry popote pale na kuzipa baridi na kula  na pia naweza kushikilia Ice cream kwa muda mrefu bila ya kuyeyuka. Ni rahisi sana mnajua hadi nashangaa”Aliongea Regina  kama vile anataka kuruka ruka.

Hamza na Shangazi walijikuta wakiangaliana  na kuonekana  wakiwa kama wamechanganyikiwa.

‘Wife , umewezaje?’

Hamza alishindwa kuelewa kabisa  na kujikuta akimwangalia  Regina kwa shauku. Regina  mara baada ya kuona walivyochanganyikiwa  alionekana kujivunia zaidi.

“Mimi sielewi ,  nilikuwa nikiwaza jambo flani hivi  ila ghafla tu  yale maandishi ni kama yamejitafsiri katika kichwa changu  na kuna sauti inaniambia nihisi  hivi kwenye moyo wangu  na mikono yangu itaonyesha matokeo na ndio kilichotokea”

“Lakini  ndio kwanza upo  levo ya nusu mzunguko ,  kuweza kutoa nishati  ya mbingu na ardhi   inaweza fanywa na mtu aliefikia levo ya nafsi  na kupata ufunuo. Wapo hata baadhi ya  watu wamefikia levo ya nafsi lakini hawajawahi pata ufunuo wa  namna ya kutoa nishati zao   nje zaidi ya kuzitawala ndani ya miili yao tu”

Hamza hakuelewa , hajawahi kusikia mahali popote pale katika mafunzo ya nishati , mtu akiwa katika levo ya  nusu mzunguko   kupata  ufunuo.

Ikumbukwe kwamba mafunzo ya nishati  ni kama mtu anavyofanya maombi , kadri uvyosali ndio unavyozidi kunyonya nguvu ya kiroho  na kukuwa kimadaraja , ukifikia daraja flani ndio sasa unafunuliwa  vitu ambavyo hukuwahi kufikiria. Sasa  Regina ambae ndio kwanza  tu ameanza kuingia katika daraja la nusu mzunguko inawezekana vipi akapata ufunuo haraka hivyo. Hata Shangazi alionekana kushangaa.

“Regina mbinu unayojifunza ndio bibi yako alijifunza pia , lakini  ulichofanya ni tofauti  kabisa na  bibi yako , alikuwa akitoa nishati lakini haikuwa ya ubaridi mkali kama wewe”Aliongea shangazi.

Hamza hata yeye aliweza kuthibitisha wasiwasi wake ,  alichotoa Regina  kilionekana kukosa  uhusiano na  ufunuo  kabisa wa kinishati. Kwasababu siku zote  nishati  ina nguvu mno  kiasi kwamba ili  mtu ahimili kutoa lazima afikie daraja la ukamilisho  wa mwili  au ukaidi wa asili , kitu ambacho Regina alikuwa mbali sana. Lakini hata hivyo  Hamza  alifikiria tofauti , aliona pengine ni kama  Nyakasura tu,  watu waliozaliwa  tayari na uwezo,  ambao unahitaji  kitu kama switch  tu kuamsha.

Hamza aliona kama ni kweli basi  anachofikiria Regina ni ujinga kutaka kutumia uwezo huo kuzipa baridi Strawberry , kwasababu kama uwezo upo ndani yake mara nyingi ni hatari kama mtu hawezi kuudhibiti na anaweza kuua mtu bila kukusudia.

“Mbona  mna  hali ya mashaka usoni , kuna kitu nimekosea?”

“Regina kuna hali mbaya unajisikia mwilini?”Aliongea Shangazi akimwangalia Regina kwa wasiwasi.

“Hapana najisikia vizuri tu , mwili wangu  ni mwepesi sana”

“Wife  kwasasa  kuna  uwezekano wa aina mbili ,  kwanza labda ile pete ndio inaonyesha athari zake kwako  au mwili wako wenyewe ulikuwa na  uwezo  ambao  umeanza kujionyesha wenyewe baada ya kuanza mafunzo. Kwasasa  hakuna uwezekano wa kujua nini kinakutokea , kama utaendelea kuhisi hakuna tofauti katika mwili wako , basi unaweza kuendelea kujifunza”

Hamza alifikiria mambo mawili kwa wakati mmoja , nishati ile  iliotoka  katika pete kumponya Regina ilikuwa pia na nguvu ya ubaridi , lakini hakutaka kuamini moja kwa moja kama  ndio imemfanya Regina kuwa na uwezo huo , pengine Regina mwenyewe ndio alikuwa na uwezo  ambao labda alizaliwa nao.

Regina mara baada ya kusikia maelezo ya  Hamza alionekana kufarijika , isitoshe alimwamini Hamza kwasababu alikuwa ni Gwiji.

“Vyovyote vile inaweza kuwa na faida kwa Regina na kwa familia kwa ujumla , leo  naenda kupika chakula  kizuri kwa ajili ya kusherehekea”Aliongea Shangazi.

“Shangazi wewe unapika chakula kingi , huna haja ya kuongezea sana”Aliongea na kumfanya Shangazi kucheka na Hamza pia.

Wakati wa chakula cha usiku Hamza alimwambia  Regina atatoka kesho   kwenda kuonana  na Irene. Hakutaka tu kuondoka kimya kimya , Regina kusikia hivyo  uso wake palepale ulionyesha hali ya kutokufurahi.

“Niko bize na kazi, lakini wewe una  hadi muda wa kusindikiza watu  matembezini , hata hivyo sitaki kujali unachofanya , unaweza kwenda tu” Aliongea Regina kwa sauti hafifu.

Hamza mara baada ya kuona amemfanya mwanamke huyo kutokuwa na furaha , alijikuta akitoa tabasamu la haya.

“Mke wangu , unaonaje baada ya chakula twende tukatembee , tunaweza kwenda kuangalia  movie na  miwani za  teknolojia mpya ya Meta?”

Hamza alikumbuka hajatoka out sana na Regina , lakini alishawahi kwenda  na Dina na  Eliza kuangalia filamu ,   lakini  muda huo alikumbuka kulikuwa na uzinduzi wa  teknolojia mpya ya  miwani  ya kampuni ya Meta ambazo zilikuwa zikitumiwa kwa mara ya kwanza katika moja ya ukumbi wa sinema Mlimani nchini Tanzania.

“Itakuwa vizuri Regina. Mnaweza kwenda kuangalia  movie , isitoshe muda  bado mapema na ukikaa nyumbani hupumziki zaidi ya kufanya kazi”Aliongea Shangazi haraka kumpigia   pasi Hamza.

Regina kusikia hivyo  aliguswa moyoni ,  ijapokuwa kuangalia  filamu   kwa Tanzania ilikuwa sio maarufu sana kama date , lakini Regina ambae alikuwa na exposure alitamani  kujaribu pia.

Mara yake ya mwisho kwenda kuangalia sinema , ilikuwa nchini Marekani na alienda na marafiki zake  waliokuwa na wapenzi wao  huko Las Vegas , ila  tokea hapo hakuwahi   tena baada ya kuchukua hatamu ya uongozi wa kampuni.

“Ni wapi tunaenda kuangalia na filamu gani  kama sio nzuri siendi?”

“Tunaenda Century Cinemax Mlimani City  ndio pazuri , filamu inaitwa the Descent”Aliongea Hamza na Regina alitingisha kichwa.

Hamza mara baada ya Regina kukubali alitamani kutoa kicheko cha furaha , lakini alijifanyisha tu kushangaa.

“Wife mbona hata huulizi ni  filamu  inayohusiana na nini? Si umesema kama ni mbaya huendi?”

Regina alijikuta akishangaa na kukumbuka   alikubali haraka haraka bila ya kufikiria.

“Jina  ndio  nimelipenda  nimeona ni nzuri , kwani ni mbaya au? Basi tusiende”

“Ni nzuri , halafu napenda nikaiangalie na wewe mke wangu”Aliongea Hamza na tabasamu.

Baada ya chakula , Regina alibadilisha  na kuvaa  vazi  la rangi ya gray  na mkoba wa Prada  mdogo. Kwa staili aliovaa hakuwa kama bosi wa kampuni kubwa kama ya  Dosam , alionekana kama mrembo ambae amemaliza chuo  na ndio anatoka date na mpenzi wake.

Uzuri  wake haukuwa ule wa vipodozi , ulikuwa ule  wa asili  na ngozi  laini iliotunzwa vizuri. Moja ya sababu ambazo zinamfanya  Regina kuvutia ni silika yake ya ukauzu  ni kama ilimwongezea hadhi ya mwanamke wa matawi.

Mara baada ya kuelekea gereji na Hamza kumuona Regina alikuwa akielekea moja kwa moja katika gari yake  , almzuia  haraka.

“Wife tunaenda date , haina haja ya kutumia  gari  la kuteka  attention ya watu , tutumie  ya mwonekano wa kawaida”

Regina aliishia kuitikia ‘ oh!’ na kisha alimfuata Hamza na kuingia kwenye   Mercedenz S65. Haikuwa gari  ya kawaida  kithamani , ilikuwa gari ya kawaida kimwonekano pekee , ila  ilikuwa ikigharimu zaidi ya  milioni mianne za kitanzania mpaka mia sita kuingiza Tanzania.

Hamza  aliendesha gari mpaka Mlimani City , mara baada ya kuingia  na kuegesha gari , alitumia simu kununua tiketi haraka haraka.

Regina ilikuwa mara yake ya kwanza kuja Ml;imani kwa ajili ya kuangalia filamu , na pia   alikuwa mgeni kwenye kutumia simu kama hivyo kununua tiketi.

‘Wife kuna siti maalumu za wapenzi , tuchukue hizi au za  kawaida?”Aliongea Hamza.

“Ndio zikoje hizo za wapenzi?”

“Tunatenganishwa na watu wengine  tunakuwa sisi tu  yaani” Aliongea Hamza huku akimkonyeza.

“Wewe,  unapanga  kufanya vitu vichafu sio?”

“Wife vitu gani vichafu , wapenzi wakiwa wanaangalia filamu , ni kawaida kufanya vitu kama kukiss , kushikana  na mengineyo , kwanini useme ni vichafu?”

“Ah! Kama ni hivyo basi siendi”

“Basi, basi mke wangu ,  hatutokaa pamoja , sitokukiss wala kukugusa , sawa?”

“Basi twende tu na hizo za wapenzi ,  nataka kujaribu kama wtu wengine”Aliongea Regina kwa sauti ndogo.

Hamza mara baada ya kusikia kauli hio  alishangaa na kujiambia   wanawake wapo kinyume nyume  wanavyoongea.

Mara baada ya kupata tiketi zao walishuka  na moja kwa moja walielekea  mlangoni ,  wakati wakielekea  ndani Regina aliona   vinywaji flani hivi vilivyohifadhiwa  kwenye shelf na vilikuwa na picha za  mtu kama Zombie huku umbo lake likiwa sio la kawaida.

“Hivyo  vinywaji ni shilingi  ngapi?”

“Elfu kumi na tano  tu dada”

“Kuna  vyenye radha ya strawberry?”

Wakati Hamza  akitaka  kuuliza kwanini  wameweka nembo  za  picha ya mazombie,  alisogea  mteja mwingine na kuongea kauli ambayo ilimshangaza Hamza kidogo.

“Dada  chungu changu kimeachwa?”Aliongea yule mteja na Hamza palepale  ni kama  kuna suala lilichipua kwenye akili yake.

Previoua Next